Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
24 March 2026, 18:41

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linaendelea na juhudi za uokoaji pamoja na kuhakikisha wananchi wanapatiwa msaada na kubaki salama wakati huu
Na Katalina Liombechi/Kuruthumu Mkata
Kaya zaidi 100 katika Wilaya ya Kilombero zimeathiriwa na mafuriko yaliyotokea usiku wa kuamkia leo, Machi 24, 2026, baada ya maji kufurika na kuingia katika makazi ya wananchi.
Kwa mujibu wa SF Haji Madulika kamanda wa jeshi la Zimamoto na uokoaji wilaya ya Kilombero amesema maeneo yaliyoathirika ni pamoja na Mabukula katika Kata ya Kibaoni, pamoja na Kata za Lumemo, Michenga na Mbasa,Kiberege Mbingu Pamoja na Chita ambapo wakazi wamelazimika kuhama kwa muda na kukabiliana na athari za mafuriko hayo.

Mkuu wa Wilaya ya Kilombero ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, Wakili Dunstan Kyobya, ametembelea maeneo hayo kwa nyakati tofauti na kuwataka wananchi kuweka kipaumbele kwenye usalama wao.
Amebainisha kuwa hadi sasa hakuna taarifa ya kifo wala madhara makubwa yaliyoripotiwa.

Kwa upande wao baadhi ya wananchi wameelezea hali hiyo na namna ilivyowaathiri.

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linaendelea na juhudi za uokoaji pamoja na kuhakikisha wananchi wanapatiwa msaada na kubaki salama wakati huu wa changamoto.
Hali inaendelea kufuatiliwa kwa ukaribu huku mamlaka zikisisitiza tahadhari kwa wakazi wa maeneo hatarishi.