Pambazuko FM Radio

Watu wenye ulemavu Ifakara walia kukosa wakalimani

2 December 2025, 9:47 pm

Picha ya Ofisi ya Afisa Ustawi wa Jamii Ifakara (Picha na Katalina Liombechi)

Inapofikia maadhimisho ya Siku ya Watu wenye Ulemavu wadau wanahimizwa kuendelea kuwekeza katika huduma jumuishi ili kuhakikisha kuwa watu wote, wakiwemo wenye ulemavu, wanapata huduma bora na stahiki bila vikwazo.

Na Katalina Liombechi

Katika kuelekea maadhimisho ya Siku ya Watu Wenye Ulemavu Duniani, Desemba 3, 2025 changamoto ya upatikanaji wa huduma shirikishi kwa watu wenye ulemavu bado inaendelea kuonekana katika maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza na Pambazuko FM, Elizabeth Luta kupitia kwa mkalimani Mwalimu Ngewe kutoka Chama cha Viziwi Wilaya ya Kilombero, amesema watu wenye ulemavu wa kusikia wamekuwa wakikumbana na ugumu mkubwa wanapohitaji huduma katika taasisi mbalimbali kutokana na ukosefu wa wataalam wa lugha ya alama.

Amesema wanapotembelea hospitali, ofisi za umma au sehemu nyingine za huduma, mara nyingi hushindwa kuelewana na wahudumu, jambo linalowafanya kukosa haki zao za msingi na kwa wakati.

Picha ya Elizabeth Luta kutoka chama cha Viziwi Kilombero(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti ya Mwalimu Ngewe Mkalimani kwa niaba ya Elizabeth Luta

Kwa upande wake Afisa Ustawi wa Jamii katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara, Freedom Crispine Lugongo, amekiri kuwepo kwa changamoto hiyo na nyinginezo zinazowakabili watu wenye ulemavu.

Ameeleza kuwa halmashauri tayari imechukua hatua mbalimbali za kukabiliana na tatizo hilo, ikiwemo kutumia lugha ya alama.

Picha ya Freedom Crispine Lugongo Afisa Ustawi Halmashauri ya Mji Ifakara(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti ya Afisa Ustawi wa Jamii Ifakara

Aidha Afisa ustawi huyo amesema licha ya kushirikiana na wadau mbalimbali,kama Halmashauri wamekuwa na bajeti ya kuwainua watu wenye ulemavu kiuchumi,kuwatambua na kuwafikia kwa huduma mbalimbali wanafunzi na hata walio nje na shule huku akitoa wito kujiunga katika vyama vya watu wenye ulemavu ili wawe na sauti ya pamoja.

Sauti ya Afisa Ustawi wa Jamii Ifakara

Maadhimisho ya siku ya watu wenye ulemavu 2025 kimkoa yanafanyika Morogoro Mjini yanakwenda na kauli mbiu isemayo “Kuendeleza jamii jumuishi kwa watu wenye ulemavu kwa mustakabali wa ustawi na jamii’’