Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
21 October 2025, 6:08 pm

Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani utafanyika siku ya Jumatano, tarehe 29 Oktoba 2025, kwa mujibu wa Kifungu cha 69(1) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya mwaka 2024
Na Amina Mrisho
Katika kuelekea uchaguzi mkuu Oktoba 29,2025 Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Kilombero, Bi. Joha Mlindwa amesema wapiga kura wataruhusiwa kushiriki zoezi hilo muhimu kikatiba hata kwa kutumia vitambulisho vingine kama vitambulisho vya kupiga kura watakuwa wamepoteza.
Akizungumza na Pambazuko FM amevitaja vitambulisho hivyo vinavyoruhusiwa kutumika kuwa ni pamoja na leseni ya udereva,pasi ya kusafiri na Kitambulisho cha Taifa NIDA huku akisisitiza kuwa majina ya kitambulisho mbadala ni lazima yafanane na yale yaliyo kwenye Daftari la kudumu la Mpiga kura.
Bi.Joha amesema vituo vilivyotumika kuandikisha wapiga kura ndivyo vitakavyotumika kupigia kura siku ya uchaguzi.
Aidha ametoa wito kwa wananchi wa jimbo la Kilombero kufika kwenye vituo walivyojiandikishia kwa ajili ya kuhakiki majina yao ambayo tayari yameshabandikwa, na zoezi hilo limeanza leo 20 oktoba 2025 hadi siku ya kupiga kura.