Boma Hai FM

RUWASSA Hai waadhimisha wiki ya maji

19 March 2026, 5:22 pm

Pichani ni mkuu wa wilaya ya Hai (aliyesimama)Hassan Bomboko akizungumza na wadau mbalimbali wa maji katika ukumbi wa RUWASSA wilaya ya Hai, kushoto ni kaimu katibu tawala wilaya ya Hai Marry Mnyawi pamoja na Kaimu Meneja RUWASSA wilaya ya Hai Mhandisi Bendict Daniel(picha na Elizabeth Mafie)

Juhudi za kulinda vyanzo vya maji zimeendelea kupewa kipaumbele wilayani Hai, huku viongozi wakisisitiza ushirikishwaji wa wananchi ili kudumisha upatikanaji wa maji safi na salama,Mafanikio ya Bodi ya Maji Uroki Bomang’ombe yamepongezwa kwa kung’ara kitaifa, wakati hatua za kudhibiti uharibifu wa miundombinu pamoja na utoaji wa elimu kwa jamii zikiendelea kuimarishwa.

Na Elizabeth Mafie

Mkuu wa wilaya  ya Hai mkoa wa Kilimanjaro Hassani Bomboko amezitaka bodi za maji wilaya ya Hai  kuendelea kulinda na kutunza, vyanzo vya maji kwa kushirikisha wananchi ili kuhakikisha huduma ya maji safi na salama inaendelea kupatikana bila vikwazo.

Pichani ni mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Bomboko akipanda mti katika chanzo cha maji Kikafu Soka katika uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya maji Kiwilaya(picha na Elizabeth Mafie)

Bomboko ametoa kauli hiyo Machi 18, 2026 alipokuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya  maji kiwilaya, yaliyofanyika katika ukumbi wa Mamlaka ya maji safi na usafi wa Mazingira (RUWASSA) wilaya ya Hai.

Pichani ni Mwenyekiti Halmashauri ya wilaya ya Hai Edmund Rutaraka (wa kwanza kushoto)akifuatilia uwasilishwaji wa taarifa kutoka bodi mbalimbali za maji.(picha na Elizabeth Mafie)

Bomboko amesema ushirikishwaji wa wananchi ni muhimu katika kulinda vyanzo vya maji, na kuonya kuwa  Iwapo zipo shughuli za kibinadamu zinazofanyika kwenye maeneo ya vyanzo hivyo zinapaswa kusitishwa mara moja ili kuepusha uharibifu.

Sauti ya mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Bomboko

Katika hatua nyingine, Bomboko ameipongeza  Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira(RUWASSA) pamoja na bodi za maji kwa juhudi zao za kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama kwani Bodi ya Maji Uroki Bomang’ombe imekuwa mfano bora, akibainisha kuwa imefanikiwa kushinda tuzo ya bodi bora mkoani Kilimanjaro kati ya bodi 35, pamoja na kutunukiwa tuzo ya kitaifa kwa utoaji wa huduma bora.

Sauti ya Mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Bomboko

Kwa upande wake,Mwenyekiti wa Halmshauri  ya wilaya ya Hai  Edmund Rutaraka, amezipongeza bodi za maji kwa kuhakikisha huduma inapatikana wakati wote licha ya changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

Pichani ni Meneja Bodi ya maji Uroki Bomang’ombe Mhandisi Anorld Mbaruku akiwasilisha taarifa ya bodi hiyo.(picha na Elizabeth Mafie)

Naye Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Hai Wanguba Maganda, amezitaka bodi hizo kutoa elimu kwa wananchi wanaoharibu miundombinu ya maji, ikiwemo kukata mabomba, na kusisitiza kuwepo kwa adhabu kali kwa waharibifu.

Akizungumzia uzinduzi huo,kaimu  Meneja wa Mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira( RUWASSA )wilaya ya Hai, Mhandisi Benedcti Daniel, amesema miti 100 imepandwa katika chanzo cha maji Kikafu Soka kama sehemu ya juhudi za kulinda mazingira na kwamba  elimu kwa wananchi itaendelea kutolewa kupitia vyombo mbalimbali vya habari.

Sauti ya kaimu  Meneja wa Mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira( RUWASSA )wilaya ya Hai, Mhandisi Benedcti Daniel,

Hata hivyo meneja wa Bodi ya Maji Uroki Bomang’ombe Mhandisi Anord Mbaruku, amesema mafanikio yao yametokana na utendaji mzuri na utoaji bora wa huduma, huku akiahidi kuendelea kuboresha huduma na kuwakumbusha wananchi kulipa ankara za maji kwa wakati.

Sauti ya Meneja bodi ya maji Uroki Bomang’ombe Mhandisi Anorld Mbaruku

Wiki ya maji huadhimishwa kote duniani kila ifikapo Machi 16 na kilele chake ni Machi 22 ambapo mwaka huu maadhimisho hayo yanatarajiwa kufanyika kitaifa mkoani Morogoro yakiongozwa na kauli mbiu isemayo”Rasilimali za maji na usawa wa kijinsia”

Pichani ni baadhi ya madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Hai wakifuatilia uwasilishwaji wa taarifa za bodi mbali mbali za maji(picha na Elizabeth Mafie)