Boma Hai FM
Boma Hai FM
6 March 2026, 1:20 pm

Ikiwa zimepita siku kumi na mbili pekee tangu ziara ya waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Mwigulu Nchemba, mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Bomboko ameendelea kusikiliza kero za wananchi wa wilaya ya Hai na kuzitatua.
Na Elizabeth Mafie & Salma Mgosso
Hai-Kilimanjaro
Mkuu wa Wilaya ya Hai mkoa wa Kilimanjaro Hassan Omar Bomboko amesema serikali itaendelea kusikiliza na kutatua kero za wananchi ili kuboresha huduma na maendeleo na kwamba utaratibu huo ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha wananchi wanapata nafasi ya kueleza changamoto zao moja kwa moja kwa viongozi.
Akizungumza katika kikao cha kusikiliza kero za wananchi Machi 5, 2026 katika viwanja vya Ofisi ya mkuu wa wilaya, Bomboko ameainisha baadhi ya kero zilizowasilishwa hapo awali ambazo ni kuhusu huduma za kijamii, miundombinu ya barabara, maji na umeme pamoja malalamiko yanayohusu mikopo, huduma za afya pamoja na migogoro ya ardhi na mirathi iliyowasilishwa na wananchi wakati wa ziara ya waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh Dkt Mwigulu Lameck Nchemba.

Bomboko amebainisha kuwa kutokana na maelekezo ya waziri mkuu ya kushughulikia kero za wananchi na kutokuzoea matatizo yao, ofisi ya mkuu wa wilaya ya Hai imeendaa utaratibu wa kusikiliza kero za wananchi kila wiki siku ya alhamis ofosini kwake na mara baada ya hapo atasilikiza kero katika tarafa zote za wilaya ya Hai lengo ikiwa ni kutatua kero hizo kwa wakati .
Katika kikao hicho wananchi walisikilizwa kero zao mojawapo ikiwa ni mgogoro wa ardhi katika shule ya msingi Gezaulole ambapo wananchi hao walilalamika kuhusu eneo wakitaka fidia ambapo mkuu wa wilaya ameagiza wananchi hao kulipwa fidia ya viwanja au wafanyiwe tathimini na wapatiwe fedha na kwamba wapo baadhi wananchi waliingilia eneo la barabara hivyo ni wajibu wao kuondoka pamoja na wale ambao tayari wamepatiwa fidia.
Katika hatua nyingine Bomboko amemtaka mkurugenzi wa Rozina Orphan Center Rozmin Njau kufuata taratibu za kusajili makao ya kuelea watoto yatima kwani malalamiko yake yanatokana na yeye kutofuata utaratibu unaotakiwa.

Kwa upande wake, diwani wa kata ya Bomang’ombe Evod Njau, amesema wananchi wa wilaya ya Hai wameanza kuyaona matunda ya ziara ya waziri mkuu Mwigulu Lameck Nchemba kwani baadhi ya kero zilizokuwa zikiwakabili wananchi zimeanza kutatuliwa.
Kwa upande wao wananchi waliotatuliwa kero zao hususani migogoro ya ardhi katika kikao hicho wamemshukuru mkuu wa wilaya ya Hai kwani kero zao zimetatuliwa kwa wakati na wanaamini zilizobaki zitapatiwa ufumbuzi.
Hata hivyo Bomboko amemtaka afisa ardhi wilaya ya Hai kumuondoa mara moja mwananchi ambae inadaiwa amelipwa fidia lakini amegoma kuachia eneo na kwamba maeneo yote ya Halmashauri yapatiwe Hati.