Boma Hai FM
Boma Hai FM
5 February 2026, 1:21 pm

Katika kuadhimisha miaka 49 ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) wananchi,wanachama pamoja na Diwani wa Kata ya Machame Kaskazini wameadhimisha siku hiyo kwa kupanda miti pamoja na kutembelea wagonjwa kituo cha afya Kisiki.
Na Bahati Chume
Hai -Kilimanjaro
Wananchi wa Kata ya Machame Kaskazini wilaya ya Hai mkoa wa Kilimanjaro wameungana kusherehekea maadhimisho ya miaka 49 ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kufanya zoezi la upandaji miti na kutembelea wagonjwa katika Kituo cha Afya Kisiki.
Zoezi hilo la upandaji miti pamoja na kutembelea wagonjwa limeongozwa na Diwani wa Kata hiyo ambae pia ni makamu mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Hai Trael Mboya februari 2,2026 kwa kushirikiana na wananchi, huku akisisitiza umuhimu wa kutunza miti hiyo ili malengo ya uhifadhi wa mazingira na maendeleo endelevu ya jamii yafanikishwe.

Hata hivyo diwani Trael Mboya ameipongeza serikali kwa kutoa fedha kwa ajili ya miradi mbalimbali ya maendeleo katika kata hiyo, ikiwemo Kituo cha Afya Kisiki, na kuahidi kufanyia kazi ombi la ujenzi wa uzio ili kuhakikisha usalama wa mali na watumishi waliopo katika kituo na kwamba matumaini yake ni kuona kituo hicho kinaendelea kupanuka ili kiweze kutoa huduma kwa wananchi wengi.
Kwa upande wake mwenyekiti wa CCM kata hiyo Amini Mushi amewahimiza wananchi kutunza miti iliyopandwa na kwamba kupanda miti pekee hakutoshi, bali usimamizi makini wa kila mmoja unahitajika ili kutimiza lengo.
Nae mganga mfawidhi wa Kituo cha Afya Kisiki Saruni Kaleya, ameishukuru serikali kwa hatua mbalimbali za kuboresha huduma za afya, ikiwemo kuongezwa kwa watumishi na kuwepo utaratibu wa Bima kwa wananchi, ili kuhakikisha kila mmoja anapata huduma kwa urahisi.

Pichani ni diwani kata ya Machame Kaskazini ambae pia ni makamu mwenyekiti Halmashauri ya wilaya ya Hai Trael Mboya(katikati) picha na Bahati Chume