Boma Hai FM

Diwani Martin Munisi azindua barabara ya Nronga, Aomba tena mita 200

19 January 2026, 1:25 pm

Pichani ni Diwani wa kata ya Machame Magharibi Martin Munisi (aliyevaa suti) akizindua barabara ya Kalali – Nronga (picha na Henry Keto)

Baada ya wananchi wa kijiji cha Nronga kupitia changamoto ya muda mrefu ya ubovu wa miundombinu ya barabara kwa sasa hawana changamoto tena baada ya barabara ya Kalali – Nronga kujengwa kwa kiwango cha zege na kuzinduliwa rasmi na Diwani wa Kata ya Machame Magharibi Martin Munisi.

Na Elizabeth Mafie na Henry Keto

Hai-Kilimanjaro

Wananchi wa Kijiji cha Nronga, Kata ya Machame Magharibi wilayani Hai mkoani Kilimanjaro, wameondokana na adha ya muda mrefu ya miundombinu mibovu  mara  baada ya kukamilika kwa ujenzi wa barabara ya Kalali – Nronga iliyokuwa kero kwa miaka mingi, hususan wakati wa mvua, hali iliyokuwa ikiwalazimu kutembea umbali mrefu kufuata barabara mbadala.

Pichani ni barabara ya Kalali-Nronga iliyojengwa kwa kiwango cha zege(picha na Henry Keto)

Wananchi wameeleza furaha yao wakisema kukamilika kwa barabara hiyo kutarahisisha usafiri na usafirishaji, kuokoa muda, kupunguza gharama za maisha pamoja na kuongeza fursa za kiuchumi, ikiwemo usafirishaji wa mazao ya kilimo na kuwafikia kwa urahisi huduma muhimu.

Sauti za wananchi wa kijiji cha Nronga.

Akizungumza mara baada ya kuzindua rasmi barabara hiyo, Diwani wa Kata ya Machame Magharibi, Mh Martin Munisi, amesema awali barabara hiyo ilikuwa korofi kiasi cha kusababisha ajali na hata kupoteza maisha, huku wananchi wakilazimika kuzunguka umbali mrefu ili kufika mjini kutokana na ubovu wake.

Sauti ya Diwani wa kata ya Machame Magharibi Martin Munisi.

Munisi ameipongeza Serikali kwa hatua hiyo, huku akiomba kukamilishwa kwa Mita  200 zilizosalia ili barabara hiyo itumike kikamilifu kwa mwaka mzima, jambo litakalowezesha wananchi wa Machame Magharibi kuendelea na shughuli zao za kiuchumi kwa urahisi na usalama zaidi.

Pichani ni Diwani wa kata ya Machame Magharibi Martin Munisi(picha na Henry Keto)
Pichani ni Diwani wa kata ya Machame Magharibi akiwa na watendaji wa kata ,viongozi wa dini,polisi kata pamoja na wananchi wa kijiji cha Nronga(picha na Henry Keto)

Akizungumza kwa niaba ya meneja wa TARURA wilaya ya  Hai  Mhandisi Christopher Deogratius amesema ujenzi wa barabara ya changarawe yenye urefu wa kilomita 6 katika maeneo ya milimani ya Kalali Nronga, pamoja na uwekaji wa mitaro na tabaka la zege katika mita 400, huku zilizotekelezwa kwa gharama ya shilingi milioni 448, fedha zilizotolewa na Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Hai.

Sauti ya Mhandisi Christopher Deogratius