Boma Hai FM

Wananchi wa Hai wakumbushwa nafasi ya lishe bora

28 November 2025, 5:15 pm

Pichani ni mkuu wa wilaya ya Hai Hassani Bomboko (kushoto)akipata maelezo kuhusu vyakula mbalimbali kutoka kwa afisa lishe wilaya Abel Mwaipungu. (picha na James Gasindi)

Siku ya Lishe Kitaifa huadhimishwa kila mwaka nchini Tanzania ili kukumbusha dhana ya haki ya kupata chakula bora, kupambana na udumavu, na kuhimiza uwekezaji katika afya dhamira inayokwenda sambamba na mpango wa taifa wa kuboresha lishe ulioanzishwa miaka kadhaa iliyopita.

Na James Gasindi Hai -Kilimanjaro

Maadhimisho ya Siku ya Lishe kitaifa yamefanyika  Kiwilaya  leo katika Kituo cha Afya Masama  kilichopo Kata ya Romu wilayani Hai, yakilenga kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa lishe bora kama msingi wa afya na maendeleo ya kiuchumi.

Siku ya Lishe Kitaifa huadhimishwa kila mwaka nchini Tanzania ili kukumbusha dhana ya haki ya kupata chakula bora, kupambana na udumavu, na kuhimiza uwekezaji katika afya dhamira inayokwenda sambamba na mpango wa taifa wa kuboresha lishe ulioanzishwa miaka kadhaa iliyopita.

Pichani ni mkuu wa wilaya ya Hai akiwa na wanafunzi waliojitokeza katika maadhimisho ya siku ya lishe yaliyofanyika katika kituo cha afya Masama kata ya Romu(Picha na James Gasindi)

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mkuu wa Wilaya ya Hai Hassan Bomboko amesema taifa linategemea wananchi kama nguvu kazi lakini mchango huo hauwezi kutimia bila afya bora. Amesema afya njema huanzia kwenye uchaguzi sahihi wa chakula na namna jamii inavyojenga utamaduni wa ulaji unaozingatia virutubisho muhimu. Ameeleza kuwa suala la lishe limekuwa ajenda ya muda mrefu ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tangu akiwa Makamu wa Rais na hadi sasa akiwa madarakani ameendelea kulipa kipaumbele ili kupunguza changamoto za kiafya katika jamii.

Bomboko amesema katika kipindi cha miaka mitano, serikali imewekeza zaidi ya shilingi bilioni 11 katika sekta ya afya wilayani Hai, uwekezaji unaoonekana katika ujenzi wa miundombinu, upatikanaji wa vifaa tiba na ufikishaji wa huduma kwa wananchi. Amesema jamii inapaswa kuunga mkono jitihada hizo kwa kuhakikisha watoto wanapata lishe bora kuanzia majumbani hadi mashuleni na wazazi kufuatilia chakula kinachotolewa shuleni ili kujiridhisha kuwa kina ubora unaohitajika.

Sauti ya Mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Bomboko.

Amesema maeneo mengi ya wilaya hiyo yana uwezekano mkubwa wa uzalishaji wa mazao na matunda mbalimbali hivyo wananchi hawana sababu ya kukosa lishe bora nakuonya kuwa ulaji usiozingatia virutubisho unaweza kusababisha magonjwa sugu yanayoweza kuathiri vizazi vinavyofuata na kuongeza gharama kubwa za matibabu. Katika tathmini ya wilaya, ameweka wazi kuwa bado kuna asilimia 32 ya watoto wenye udumavu jambo linaloonyesha uwepo wa pengo la uelewa na uhitaji wa kampeni endelevu za lishe.

Pichani ni mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Bomboko (aliyevaa kofia) akiwa na halmashauri ya wilaya ya Hai katika maadhimisho ya siku ya lishe(picha na James Gasindi)

Afisa Lishe wa Wilaya ya Hai Silvania Kulaya amesema wanaume wanapaswa kushiriki kikamilifu katika shughuli za lishe kwa kuwa wao ndio waamuzi wakuu katika matumizi ya rasilimali za familia. Amesema halmashauri imeendelea kuanzisha programu za lishe, kutoa elimu katika vituo vya afya, mashuleni na kwenye makundi ya kijamii ili kupunguza changamoto za utapiamlo kwa watoto na wanawake.

Sauti ya afisa lishe wilaya ya Hai Slivania Kulaya

Baadhi ya wananchi akiwemo Juleth Swai, Mc Shuma na Zaina Mushi wamesema elimu waliyopata imewasaidia kubaini makosa waliyokuwa wakiyafanya katika mfumo wao wa ulaji. Wamesema mara nyingi wamekuwa wakila kwa mazoea bila kuzingatia virutubisho vinavyohitajika na sasa wameamua kubadilika na kuwa mabalozi wa kuhamasisha jamii kuhusu lishe bora.

Sauti ya wananchi waliodhuria katika maadhimisho ya siku ya lishe yalifanyika katika kituo cha afya Masama kata ya Romu.

Maadhimisho ya mwaka huu yameendelea kuikumbusha jamii kuwa lishe sio suala la anasa bali ni nyenzo ya msingi ya kujenga taifa lenye afya, nguvu kazi imara na uchumi endelevu yakiwa na kauli mbiu inayosema afya ni mtaji wako zingatia unachokula.