Boma Hai FM

Mafunzo ya jeshi la akiba ni maandalizi ya ulinzi wa Taifa-DC Bomboko

10 June 2025, 9:08 pm

Pichani ni Mkuu wa Wilaya pamoja na Viongozi wa serikali ya wilaya ya Hai wakiwa na wakufunzi wa mafunzo ya jeshi la akiba (Picha na James Gasindi)

Ufunguzi wa mafunzo ya Jeshi la akiba katika kijiji cha Kware kata ya Masama Kusini wilaya ya Hai Mkoani Kilimanjaro

Na James Gasindi. Hai-Kilimanjaro

Mkuu wa Wilaya ya Hai, Haasan Bomboko, amewataka vijana waliojiunga na mafunzo ya Jeshi la Akiba kuwa mfano wa uzalendo, uaminifu, na nidhamu ndani ya jamii wanazotoka, huku akisisitiza kuwa mafunzo hayo ni hatua ya awali ya kuandaliwa kwa ajili ya kulitumikia taifa.

Akizungumza katika kijiji cha Kware leo wakati wa uzinduzi wa mafunzo ya Jeshi la Akiba kwa vijana, DC Bomboko alisema kuwa nafasi hiyo si ya kawaida, bali ni mwito wa kuitumikia nchi kwa uadilifu na moyo wa kujitoa, pia amewaasa kuwa askari wa Jeshi la Akiba anatakiwa awe mtu anayeaminika na kukubalika na jamii, na kamwe hawezi kupata heshima hiyo bila kuwa muadilifu.

Sauti ya Mkuu wa Wilaya ya Hai Hassan Bomboko akizungumza na wananfunzi wa jeshi la akiba wakati wa uzunduzi wa mafunzo ya jeshi hilo katika kijiji cha Kware wilayani Hai
Pichani ni Mkuu wa Wilaya ya Hai Hassan Bomboko Pamoja na viongozi wa serikali ya wilaya akizungumza na wanafunzi wa jeshi la akiba wilaya ya Hai (Picha na James Gasindi)

Katika maelezo yake, Bomboko aliweka wazi kuwa sifa ya kwanza kwa mwanajeshi ni nidhamu, na kwamba mtu asiye na nidhamu hawezi kuwa askari. Alionya dhidi ya kujihusisha na vitendo vya uhalifu au kuwalinda wahalifu, akisema hilo linakiuka misingi ya maadili ya kijeshi, aidha aliwataka vijana hao kuwa mstari wa mbele katika kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kushiriki uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika hivi karibuni.

DC Bomboko aliwataka vijana kutumia kipindi chote cha mafunzo kujijenga kiakili na kiroho ili kuwa raia bora, akisisitiza kuwa maarifa yatakayopatikana yasitumike vibaya, bali yatumike kwa faida ya jamii.