Boma Hai FM
Boma Hai FM
24 March 2026, 12:12

Kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha nchini, zaidi ya kaya 500 katika kata ya Kia wilayani Hai mkoani Kilimanjaro zimekumbwa na mafuriko yaliyosababisha baadhi ya wananchi kuyahama makazi yao na kuathiri shughuli za kijamii na kiuchumi, huku wakazi wakieleza kuwa mabadiliko ya miundombinu ya makalavati katika barabara ya Moshi -Arusha yamechangia kuongezeka kwa mtiririko wa maji kuelekea maeneo ya chini, hali iliyosababisha wanafunzi kushindwa kwenda shule na biashara ndogo ndogo kusimama, wakati mamlaka husika zikiahidi kuchukua hatua za kudhibiti tatizo hilo.
Na Elizabeth Mafie
Hai – Kilimanjaro
Kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha hapa nchini, wananchi wa kata ya kia wilayani Hai mkoani Kilimanjaro wamekumbwa na athari za mafuriko yaliyosababisha zaidi ya kaya 500 kuathirika.
Taarifa kutoka eneo hilo zinaeleza kuwa baadhi ya wakazi wamelazimika kuyahama makazi yao baada ya maji kujaa katika nyumba zao, hali inayosababisha usumbufu mkubwa wa maisha na kuhatarisha usalama wao.
Wakizungumza kuhusu hali hiyo Machi 23,2026 wananchi wa kata ya Kia wameeleza kuwa changamoto kubwa inayochangia mafuriko hayo ni ukarabati unaoendelea wa makalavati katika barabara kuu ya Moshi –Arusha ambapo umebadilisha mwelekeo wa maji na kusababisha maji mengi kutoka wilaya za Siha na Arumeru kuelekezwa katika maeneo ya chini,hasa kata ya Kia .
Akizungumza baada ya kutembelea maeneo yaliyoathirika, Mbunge wa jimbo la Hai Saashisha Mafuwe amesema mafuriko hayo yameathiri kwa kiasi kikubwa shughuli za kijamii na kiuchumi, ikiwemo wanafunzi kushindwa kufika mashuleni pamoja na kusimama kwa shughuli ndogo ndogo za kiuchumi.
Ameeleza kuwa maboresho ya miundombinu ya makalavati katika eneo la mjooroni yamechangia mabadiliko ya mtiririko wa maji, hali iliyosababisha maji kuelekezwa kwa wingi katika maeneo ya chini na kuongeza ukubwa wa tatizo hilo.
Kwa upande wake Meneja Wakala wa Barabara (TANROADS) mkoa wa Kilimanjaro Mhandisi Motta Kyando amesema zipo hatua mbalimbali watakazochukua ili kukabiliana na changamoto hiyo pamoja na kutoa tahadhari kwa wananchi wanaoishi katika maeneo hatarishi.
Wakati huo huo, vijiji vya Mtakuja na Tindigani vinaendelea kuathirika na mafuriko yanayotokana na bwawa la Kidawashi lililopo wilaya ya Simanjiro, huku kijiji cha Sanya Station nacho kikikumbwa na maji yanayotoka wilaya za Siha na Arumeru.

Katika hatua nyingine Saashisha amesema tayari amewasiliana na mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro kuhusu tatizo hilo, ambapo ameahidi kuunda tume ndogo ya uchunguzi itakayofuatilia chanzo cha mafuriko hayo na kupendekeza suluhisho la kudumu.
