Boma Hai FM

TYC yawanoa vijana Kilimanjaro kuhusu umiliki wa ardhi

18 August 2024, 9:55 am

wakili Masalu Luhula akiendelea kutoa mafunzo kwa washiriki(picha na Elizabeth Mafie)
Washiriki wakisikiliza mafunzo(Elizabeth Mafie)
Mratibu wa mradi wa boresha maisha ya vijana nchini Tanzania aliyevaa shati jeupe Yahaya Kitogo akikabidhi kitabu cha mwongozo kwa mratibu wa mradi huo kwa mkoa wa Kilimanjaro Stanley Jeremia (picha na Elizabeth Mafie)
Mratibu wa mradi wa boresha maisha ya vijana nchini Tanzania aliyevaa shati jeupe Yahaya Kitogo akikabidhi kitabu cha mwongozo kwa mnufaika wa mradi huo kutoka kikundi cha Light kilichopo wilayani Hai mkoa wa Kilimanjaro Veronica Lema(picha na Elizabeth Mafie)

Tyc wameendelea kuwajengea uwezo vijana mbalimbali nchini Tanzania katika mikoa minne ambayo mradi wa Boresha maisha kwa vijana unatekelezwa.

Na Elizabeth Mafie

Shirika la Tanzania Youth Coalition (TYC) limeendelea kuwajengea uwezo vijana mbalilmbali katika mkoa wa Kilimanjaro kupitia mradi wa Boresha maisha wenye lengo la  kuwaongezea uwezo katika kuendesha mashirika yanayoongozwa na vijana hao,kuweza kukabiliana na ukatili wa kijinsia , pamoja na kuwa na uelewa kuhusu umiliki wa aridhi na namna bora ya kutumia aridhi hiyo.

Shirika hilo limefanya mafunzo kuhusu mifumo ya kisheria pamoja na haki za umiliki wa ardhi  August 15 2024  katika ukumbi wa chuo cha uhamiaji Moshi mjini mkoani Kilimanjaro na kihudhuriwa na vijana wapatao ishirini na tano wanaotoka katika vikundi mbalimbali.

Yahaya Kitogo ambae  ni mratibu wa mradi wa Boresha Maisha ya vijana nchini Tanzania amesema wamekuwa na mafunzo endelevu kuhusu mada mbali mbali  kwa vijana ambao wananufaika na mradi huo katika mkoa wa Kilimanjaro  na katika mkoa wa Mwanza, Dodoma na Iringa na kwamba kwa sasa wameona ni vyema vijana hao kujengewa uwezo  kuhusu  mifumo ya  kisheria pamoja na  haki za umiliki wa ardhi nchini Tanzania kwa kuwa vijana hao wanajihusisha na kilimo  hivyo ni vyema  kujua sheria zinasemaje  na namna ya kuweza kuwa wamiliki wa ardhi.

Sauti ya Yahaya Kitogo mratibu wa mradi nchini Tanzania

Kitogo ameongeza kuwa shirika hilo linalenga kuwafikia vijana mia tano kwa mkoa wa Kilimanjaro na kwa nchi nzima wanatarajia kuwafikiwa vijana 11,606 kupitia makundi mbalimbali ya vijana wakulima na wanaojihusidha na shughuli za ubunifu na kwamba  katika mwaka huu wa pili wa utekelezaji wa mradi wamefanikiwa kuwafikia vijana 1788 ikiwemo vikundi vya  vijana 100  katika mikoa ambayo mradi huo unatekelezwa.

 Nae  mratibu wa mradi huo katika  mkoa wa Kilimanjaro  Stanley Jeremia amesema kwa kuwa ni ngumu  kuwafikia vijana  wengi kwa wakati mmoja  wameona ni vyema kuwajengea uwezo viongozi wa vikundi na masharika ambapo wao wanakwenda kuwapatia elimu  wanachama wao kwenye vikundi na kwenye taasisi.

Sauti ya mratibu wa mradi kwa mkoa wa Kilimanjaro Stanley Jeremia

Aidha wakili na mtaalamu  wa masuala ya ardhi  kutoka Tala ambae alikuwa mkufunzi  wa mafunzo hayo  Masalu Luhula amesema kuwa vijana wengi hawana uelewa wa kutosha kuhusu utawala wa ardhi hivyo anaamini kupitia mafunzo hayo vinaja hao watapata kujua zaidi kuhusu  utawala wa ardhi   na kuitumia vizuri  kwa kupitia vikundi au mtu mmoja mmoja  kwa lengo la kuchangia katika uchumi.

Sauti ya wakili na mtaalamu wa maswala ya ardhi Masalu Luhula

 Kwa upande wao wanufaika  wa mradi huo  Joseph Godfrey  na Veronica lema wamesema kuwa shirika la Tanzania Youth coalition(TYC) limekuwa msaada mkubwa kwa vijana kutokana na mafunzo mbalimbali ambayo wamekuwa wakipatiwa kwani yamefanya vikundi vyao viwe na uelewa wa maswala mbalimbali kama vile usawa wa kijinsia,namna ya kufanya kilimo chenye tija,namna ya kumiliki ardhi na kuitumia na kwamba vijana wengine wanapaswa kujiunga na vikundi ili kupata fursa hapa nchini.