Highlands FM
Highlands FM
17 July 2025, 12:04

Walimu wametakiwa kuongeza weledi katika utendaji kazi wao ili kuepukana na vitendo vya ukatili kwa wanafunzi.
Na Samwel Mpogole
Walimu wametakiwa kuongeza weledi katika utendaji kazi wao, pamoja na kuachana na vitendo vya ukatili na unyanyapaa kwa wanafunzi, ili kuimarisha mazingira ya kujifunzia na kulea kizazi bora.
Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Beno Malisa, wakati akifungua mafunzo ya sayansi, hisabati na TEHAMA kwa walimu wa shule za sekondari, yanayofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Ualimu Rungwe.
Katika hotuba yake, RC Malisa amesema kumekuwa na matukio mengi ya walimu kujihusisha na vitendo visivyofaa, ikiwemo ukatili kwa wanafunzi, jambo linalochafua taswira ya taaluma ya ualimu na kukwamisha jitihada za kuinua kiwango cha elimu.
Kwa upande wake, Robert Msigwa, Mratibu wa Mradi wa Kuboresha Elimu ya Sekondari nchini (SEQUIP) Kutoka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa TAMISEMI amesema lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo walimu katika ufundishaji wa masomo ya sayansi na TEHAMA, ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia na mahitaji ya sasa ya soko la ajira.
Kwaupande wao baadhi ya washiriki wameeleza kuwa mafunzo hayo yamekuja wakati muafaka, na kwamba yatawasaidia kwa kiasi kikubwa kuongeza ufanisi na maarifa ya kisasa katika ufundishaji.
