Highlands FM
Highlands FM
13 June 2025, 12:05

Mbeya yazindua Mpango Mkakati wa Maendeleo 2025–2030 kufungua ukurasa mpya wa maendeleo jumuishi
Na Samwel Mpogole
Halmashauri ya Jiji la Mbeya imezindua rasmi Mpango Mkakati wa Maendeleo kwa kipindi cha miaka mitano ijayo, 2025 hadi 2030, katika hafla iliyofanyika jijini Mbeya na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, wadau wa maendeleo na wananchi.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, mgeni rasmi ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Beno Malisa, amesema mpango huo utafungua ukurasa mpya wa maendeleo kwa Jiji la Mbeya kwa kuleta mageuzi makubwa katika sekta mbalimbali.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Mbeya, AnnaMary Joseph, akimuwakilisha Mkurugenzi wa Jiji John Nchimbi, ameeleza kuwa utaratibu wa kuwa na mpango mkakati wa miaka mitano umekuwa ukitumika kama njia ya kuweka mifumo thabiti ya kuongoza jiji.
Naye Kaimu Afisa Mipango wa Mkoa wa Mbeya, Ndiyo Mwakibuka, amepongeza Halmashauri ya Jiji kwa kutekeleza agizo la serikali la kuwa na dira ya maendeleo kwa kila taasisi.
Mpango Mkakati huo wa miaka mitano unatarajiwa kuwa nyenzo muhimu ya kuongoza mwelekeo wa Jiji la Mbeya katika kukuza uchumi, kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi, na kuchochea ushiriki wa jamii katika maendeleo ya jiji.