Huheso FM

Dkt. Mzava awataka walimu kutoa malezi bora kwa wanafunzi shuleni

March 8, 2024, 3:58 pm

Mbunge wa Viti maalum Mkoa wa Shinyanga, Christina Mzava katikati mwenye miwani katika matembezi ya kuelekea shule ya msingi Nyashimbi ambapo ameahidi kutoa madawati 20.

Walimu wilayani Kahama mkoani Shinyanga wametakiwa kuwalea wanafunzi katika mienendo mizuri ili kupambana na mmomonyoko wa maadili unaoendelea kushamili nchini.

Na Neema Nkumbi-Huheso FM

Wito huo umetolewa na mbunge wa viti maalum mkoani Shinyanga Dkt. Christina Mzava alipotembelea Shule ya msingi nyashimbi iliyopo Kata ya Mhongolo Wilayani Kahama ambapo amesema walimu wana nafasi kubwa kimalezi kwani ndio wanaokaa na wanafunzi  muda mrefu.

Aidha ameongeza kuwa matukio ya mmomonyoko wa maadili yanazidi kuongezeka ikiwemo ndoa za jinsia moja, ulawiti na nyinginezo ambazo ni kinyume na maadili ya Mtanzania huku akiwataka wazazi na walezi wa watoto kukumbuka majukumu waliyopewa na muumba ya malezi badala ya kuwaachia jukumu hilo wasichana wa kazi.

Sauti ya Christina Mzava akizungumzia kuhusu mmomonyoko wa maadili nchini

Sambamba na hilo Mbunge huyo ametoa ahadi ya Madawati 20 yenye thamani ya shilingi milioni moja na laki sita ili kupunguza adha ya ukosefu wa madawati katika shule hiyo ambapo madarasa mawili hayana madawati hali inayopelekea wanafunzi kubadilishana muda wa kuingia shuleni.

kwa upande wake mwalimu mkuu Lutelemla John amemshukuru mbunge pamoja na UWT kwa kufika shuleni hapo na kueleza kuwa anakabiliwa na uhaba wa madawati ambapo vyumba viwili vya madarasa havina dawati hata moja, pia vyumba vya madarasa havitoshi hali inayopelekea darasa la kwanza na la pili wasome kwa kupokezana.

Shule ya msingi Nyashimbi ni shule iliyopo katika mtaa wa Mhongolo Kata ya Mhongolo manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga na ina wanafunzi takribani 1800 licha ya kwamba uandikishaji wa wanafunzi wa darasa la kwanza unaendelea na inakabiliwa na uhaba wa madarasa manne, na madawati 300 ambapo takribani madawati 124 yametolewa na halmashauri ya manispaa ya Kahama.