Huheso FM

Mawe ya dhahabu yakamatwa yakitoroshwa kutoka mgodi wa Bulyanhulu

August 23, 2023, 2:15 pm

Kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga, Janeth Magomi akionesha vitu mbalimbali vilivokamatwa

Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limekamata mawe yenye madini ya dhahabu yenye uzito wa gramu 6753.4 na thamani ya Tsh. Milioni 9 yakitoroshwa kutoka kwenye mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu wilayani Kahama huku pia likikamata Carbon yenye mchanga wenye madini yadhaniwayo kuwa ni dhahabu yenye uzito wa kg 261 ambayo thamani yake bado haijajulikana katika maeneo ya Manzese Kahama.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo Jumatano Agosti 23,2023 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi amesema mali hizo zimekamatwa kwa kipindi cha kuanzia tarehe 26/07/2023 hadi tarehe 22/08/2023 baada ya kufanya misako na doria katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Shinyanga.

“Pia tumekamata jumla ya lita 603 za mafuta aina ya Diesel katika maeneo tofauti ya mradi wa Reli ya mwendokasi SGR. Mafuta haya yamewekwa kwenye chupa ndogo, wezi wa mafuta sasa hivi wamebuni mbinu ya kutumia vichupa badala ya madumu makubwa”,amesema Kamanda Magomi.

Amesema , katika misako hiyo Jeshi la polisi Shinyanga pia limefanikiwa kukamata Bunduki aina ya Riffle yenye namba 2/49PF78701 ambayo ilikuwa inatumika katika shughuli za ulinzi bila kibali.

Vitu vingine vilivyokamatwa na jeshi la polisi ni madawa ya kulevya aina ya Bangi yenye uzito wa Kg 71, seti moja ya computer, Pikipiki 03, tiles Box 14, mabomba 06 ya chuma na vipande 09, Mabati 17, Plastic 3 za rangi ya majumba, mifuko 02 ya Cement, mifuko 7 ya chokaa, pamoja na Packet 120 za vipodozi vinavyoaminika kuwa na sumu.

Kamanda Magomi amesema, jumla ya watuhumiwa 31 wanashikiliwa katika vituo mbalimbali vya Polisi kuhusiana na makosa hayo na wengine wamepewa dhamana huku wakisubiri kufikishwa mahakamani.

Kwa upande wa mafanikio mahakamani,Kamanda Magomi ameeleza kuwa jumla ya kesi 34 zilipata mafanikio mahakamani ambapo kesi 5 za kubaka zilihukumiwa vifungo kati ya miaka 30 na pia kifungo cha nje miezi 12 kwa kesi za watoto (juvenile), kesi 01 ya kulawiti ilihukumiwa kifungo cha maisha Jela, kesi 02 za uvunjaji zilihukumiwa vifungo vya miezi 6, kesi 03 za ukatili kwa watoto zilihukumiwa vifungo vya miaka 05 jela, kesi 01 ya kusafirisha madawa ilihukumiwa kutumikia jamii kwa miaka 03, kesi 05 za wizi zilihukumiwa vifungo vya miezi 06 hadi mwaka 01 jela, kesi 01 ya kumtorosha mwanafunzi ilihukumiwa kifungo cha miaka 03 jela, kesi moja ya kuharibu mali ilihukumiwa kifungo cha mwaka 01 jela na kesi 01 ya kukiuka masharti ya leseni ya biashara ilihukumiwa faini ya Tsh. 500,000/=.

Kwa upande wa usalama barabarani, amesema jumla ya makosa 4017 yalikamatwa ambapo magari 3084 yalikamatwa kwa makosa mbalimbali ikiwemo kutokuwa na leseni 07, kutokuwa na Bima 179, Mwendokasi 637, kuzidisha abiria 422 na makosa mengine madogomadogo ni 588.

“Makosa ya pikipiki yalikuwa 933 ambapo kutokuwa na leseni 228, kutokuwa na Bima 164, kuzidisha abiria 121, kuendesha pikipiki bila kofia ngumu 229, kuendesha pikipiki mbovu 64, na makosa mengine ya pikipiki ni 127”,amesema Kamanda Magomi.

“Jeshi la Polisi mkoa wa Shinyanga linapenda kuwaasa wananchi wote kwa ujumla kufuata sheria za nchi na pia kutoa ushirikiano kwa Jeshi ili kudumisha amani na utulivu uliopo”,ameongeza Kamanda Magomi.