Huheso FM

Watu wawili wanashikiliwa na polisi kwa kutengeneza silaha, Shinyanga

March 27, 2024, 12:35 pm

Kamanda wa Jeshi la polisi mkoani Shinyanga, Janeth Magomi akionesha silaha zilizokamatwa

“Pia mnamo tarehe 17/03/2024 huko maeneo ya Kijiji cha Bugomba “A”, Kata ya Ulewe, Tarafa ya Mweli Wilaya ya Kipolisi Ushetu na Mkoa wa Shinyanga Jeshi la Polisi lilimkamata mtuhumiwa mmoja na baada ya kupekuliwa nyumbani kwake alikutwa akiwa na silaha 02 aina ya Gobole zisizo na namba ya usajili, Risasi 03 za Gobole, Ganda 01 ya risasi ya gobole, mafuta ya kusafishia Bunduki na Unga udhaniwao kuwa ni Baruti akiwa amevihifadhi chumbani kwake bila kibali kitu ambacho ni kinyume na Sheria za Nchi yetu”,

Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limekamata silaha tano pamoja na watuhumiwa wawili kwa kosa la kutengeneza na kumiliki silaha kinyume na sheria huku likikamata vitu mbalimbali zikiwemo bhangi, vitanda, magodoro , yai la mbuni na mkia wa nyumbu.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo Jumatano Machi 27,2024, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga SACP Janeth Magomi amesema mnamo tarehe 13/03/2024 huko maeneo ya Kitongoji cha Izagala, Kijiji cha Ntundu, Kata ya Busangi, Tarafa na Wilaya ya Kipolisi Msalala Mkoa wa Shinyanga ambapo Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga lilifanikiwa kumkamata mtuhumiwa mmoja akiwa na mtambo wa kutengenezea silaha uitwao Vice.

Kamanda Magomi ameeleza kuwa mtuhumiwa huyo pia alikamatwa akiwa na Silaha tatu aina ya Gobole, maganda matano ya risasi ya kutengeneza kienyeji, maganda manne ya Shotgun, vipande saba vya chuma na mbao mbili za kutengeneza silaha aina ya gobole.

 Amesema watuhumiwa wote wawili mara baada ya upelelezi kukamilika watafikishwa mahakamani kwa hatua zaidi za kisheria.

Akielezea kuhusu Kesi mahakamani, Kamanda Magomi amesema jumla ya kesi 13 zimepata mafanikio ambapo, kesi 02 za kubaka washtakiwa wawili walihukumiwa kifungo cha miaka 30 jela, kesi 02 za wizi washtakiwa wawili walihukumiwa kifungo kati ya miezi 06 mpaka miaka 07 jela, kesi 01 ya kupatikana na bhangi mshtakiwa alihukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela, kesi 01 kuvunja nyumba usiku na kuiba washtakiwa 02 walihukumiwa kifungo cha miaka miwili jela, kesi 06 kuingia kwa jinai washtakiwa 06 walihukumiwa kifungo cha miezi mitatu jela na kesi 01 kutishia kuua kwa maneno mshtakiwa mmoja alihukumiwa kwenda jela miezi 03.

“Vilevile Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga kitengo cha Usalama barabarani limefanikiwa kukamata jumla ya makosa 3,315 ambapo makosa ya magari ni 2,615 na makosa ya bajaji na pikipiki ni 700 wahusika waliwajibishwa kwa kulipa faini za papo kwa hapo”,amesema.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga linatoa wito kwa wananchi kuacha mara moja vitendo vya kihalifu na vilivyo kinyume na Sheria na halitasita kumchukulia hatua mtu yeyote atakayejihusisha na vitendo vya namna hiyo.