Huheso FM

Wazazi Nyahanga wahamasishana ujenzi wa vyoo shuleni

September 13, 2023, 2:51 pm

This image has an empty alt attribute; its file name is 1-450x1024.jpg
Kaimu mwenyekiti Mtaa wa Nyahanga Manispaa ya Kahama, Michael Kulwa

Na Paul Kayanda-Kahama

WAZAZI na walezi katika Mtaa was Nyahanga Manispaa ya Kahama Mkoani Shinyanga, wameombwa kuhamasika katika suala la uchangiaji wa ujenzi wa choo cha wavula kulingana na upungufu mkubwa uliopo.

Kaimu mwenyekiti wa kamati ya shule ya msingi Nyahanga ‘A’, Michael Kulwa  akizungumza na waandishi wa Habari September 12,2023 amesema kuwa kikao Cha tarehe 1,9,2023 wazazi walikubaliana kuchangishana shilingi 2700 Ili kukamilisha ujenzi wa matundu 14 ya cho cha wavulana katika shule ya msingi Nyahanga A.

Amesema kuwa shule hiyo  inazaidi ya watoto 1000 na mapungufu ni matundu 22 ya vyoo vya wavulana na hata kwa wasichana na kuongeza kuwa katika kikao hicho waliwekeana ahadi kuwa mpaka kufikia tarehe  18,2023 choo hicho kiwe kimekamilika Ili kitumike Kwa kuwa shule zitakuwa tayari zimefunguliwa.

Aidha kaimu mwenyekiti huyo amesema kuwa pamoja na mwitikio mzuri wa wazazi katika kuchangia ametumia fursa ya vyombo vya Habari kuiomba Halmashauri ya Manispaa kuunga mkono juhudi za wazazi katika umaliziaji wa maboma ya shule lakini pia ujenzi wa vyoo shuleni hapo ili kutokatisha tamaa wazazi hao.

Katika hatua nyingine wazazi hao wanashangaa kuona gulio linavamia eneo la shule hiyo ambapo wajasiriamali wameanza kuendesha shughuli zao.

“Kama mzazi na mwananchi sijui chochote kuhusu  gulio hilo tunaona shughuli zinaendelea kwenye eneo la shule,” amesema Kulwa.

Mkazi mwingine wa mtaa wa Nyahanga, Josephine Kilimba naye amesema kuwa kwenye kikao Cha wazazi shuleni hapo kipindi Cha mwezi wa nane kilichohusu kusomewa mapato na matumizi juu ya ujenzi wa choo ambapo ililetwa hoja ya kuhama kwa mnada kutoka jirani na ofisi za serikali ya mtaa na kwenda kwenye eneo la shule.

Kilimba amesema kuwa alisimama na kupinga hoja hiyo na kudai kuwa wakazi wa mtaa wa Nyahanga wnahitaji kupata shule ya Sekondari ili kuepusha watoto kuvuka barabara ya lami kwenda shule ya Sekondari Seeke.

Aidha mzazi huyo katika kikao hicho alipendekeza     badala ya kuweka mnada kwenye eneo la shule badala yake pajengwe shule ya Sekondari Nyahanga, Ili kuepusha ajari na kuongeza kuwa itakumbukwa wazazi walichangishwa fedha za ujenzi wa shule ya sekondari Kishimba, Nyihogo,Nyasubi pamoja na Busoka.

” Wazazi tunashauri kuwa ni vizuri mnada uboreshwe hapohapo, eneo la shule likaachwa ili lijengwe shule ya Sekondari, lakini Mimi nikashangaa kuona baadaye miti imesimikwa kwenye eneo la shule bila kujua ni kikao gani kingine wazazi tumeketi kukubaliana hilo na kama wananchi tunataka eneo hilo liachwe wazi Ili kujengwe Sekondari na soko lirudi lilikokuwa,” amesema Kilimba mkazi wa Nyahanga.

Pia mwananchi huyo amesema kuwa kulingana na ukuaji wa Mji wa Kahama kutaanzishwa Kata nyingine kama Shunu ambako ujenzi wa Sekondari ya Nyahanga kwenye eneo la Mtakuja unaendelea kwamba ikitokea hivyo Nyahanga haitakuwa na shule.

Naye mwenyekiti wa Mtaa wa Nyahanga Bernad Mapalala  akizungumza na mwandishi wa habari hizi Kwa njia ya simu yake ya kiganjani alisema kuwa gulio Hilo lipo kwa muda tu wakati ufumbuzi wa Soko lingine ukiendelea.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Nyahanga Pancras Ikongoli katika mahojiano maalumu na mwandishi wa Habari hizi alifafanua kuwa shule ya Sekondari inajengwa katika mtaa wa Mtakuja Kata ya Nyahanga takribani kilometa 20 kutoka mtaa wa Nyahanga na kwamba kiasi Cha shilingi Milioni 600 fedha za Rais  Samia Suluhu Hassan kilitengwa kwenye kata hiyo Ili kusaidia ujenzi huo.

Diwani Ikongoli alisema kuwa shule hiyo ipo katika hatua za mwisho na kwamba mpaka mwezi Oktoba ujenzi huo utakuwa umekamilika.

Kuhusu suala la gulio kuhamishiwa katika eneo  shule diwani huyo alisema kuwa wajasiriamali wamerahisishiwa kwa kusogezewa huduma hiyo karibu na barabara na kwa sasa na eneo Hilo ni bavazone ambapo ni hifadhi ya barabara inayomilikiwa na Wakala wa Barabara nchini(TANROADs) na kuongeza kuwa gulio Hilo lipo kwenye jaribio na ikiwa rasmi suala hilo litazungumzwa kwenye vikao vya hadhara.

Suala la gulio hilo  linaonekana kuwa ni endelevu kutokana na uboreshwaji wa  miundombinu ya vyoo pamoja na ujenzi wa vibanda kwenye eneo hilo linalodaiwa kuwa ni eneo la shule.