Huheso FM

Nyonyo kuanguka chanzo cha unyonyeshaji duni Ushetu

8 August 2024, 4:01 pm

Jamii katika halmashauri ya Ushetu wilayani Kahama mkoani Shinyanga imetakiwa kuachana na imani potofu zinazochangia uwepo wa unyonyeshaji duni hali inayosababisha utapiamlo kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano.

Kauli hiyo imetolewa na mgeni rasmi ambaye ni diwani wa Kata ya Uyogo, Joseph Bundala akimuwakilisha Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Hadija Kabojela katika kilele cha Maadhimisho ya wiki ya Unyonyeshaji yaliyofanyika Agosti 7, 2024 ambapo amewataka wataalum wa afya kuwasaidia akinamama kwa kuendelea kutoa elimu ya umuhimu wa kunyonyesha watoto ili kuodokna na udumavu wa akili na mwili.

Sauti ya mgeni rasmi Joseph Bundala akizungumza wakati wa maadhimisho ya kilele ya wiki ya unyonyeshaji

Awali, akisoma taarifa kwa mgeni rasmi, Afisa lishe wa Halmashauri ya Ushetu Khadija Nasibu amesema katika tafiti walizozifanya hivi karibuni wamebaini kuwa kati ya watoto kumi ni wanne mpaka watano wanaonyonyeshwa ipasavyo na hii ni kutokana na uwepo wa imani potofu kwa baadhi ya jamii, na mtindo wa maisha kuwa mama akinyonyesha mtoto Nyonyo zake zitaanguka/kuelegea

Sauti ya Afisa lishe halmashauri ya Ushetu akisoma taarifa ya hali ya unyonyeshaji watoto

Kwa upande wao baadhi ya akinamama wa Kata ya Uyogo wakizungumza baadaya maadhimisho hayo kwa nyakati tofauti, wamesema vijana wa siku hizi hawazingatii taratibu za afya ya uzazi hali inayosababisha watoto kupata udumavu, kwa kutokunyonyeshwa kwa kipindi cha miaka miwili na pasipo kulishwa vyakula vya makundi yote pamoja na kuhofia mabadiliko ya miili yao.

Sauti ya akinamama wakizungumzia sababu zinazosababisha hali ya unyonyeshaji kuwa duni

Hata hivyo, kutokana na matokea ya utafiti wa afya ya uzazi yaliofanyika mwaka 2024 kitaifa imebainika kuwa watoto walionyonyeshwa maziwa ya mama pekee chini ya umri wa miezi sita ni asilimia 64 %, huku utafiti huo ukionyesha kuwa watoto walionyonyeshwa kwa miaka miwili ni asilimia 37%.