Radio Jamii Kilosa

TASAF yaleta mafanikio Kilosa, wanufaika waomba kuendelezwa

19 August 2025, 11:38 pm

Baadhi ya wanufaika wa mradi wa Tasaf katika Kijiji cha Batini kilichopo kata ya Rudewa wakiwa kwenye kituo cha malipo. Picha na Asha Madohola

Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini (TASAF) ni mradi wa Serikali ya Tanzania unaolenga kusaidia kaya zenye hali duni za kiuchumi kwa kuwapatia ruzuku ya fedha, fursa za ajira za muda na kuwajengea uwezo wa kujitegemea na mradi huu umejikita katika kuboresha maisha ya walengwa kupitia miradi ya kijamii, uundaji wa vikundi vya akiba, na kusaidia mahitaji muhimu kama elimu, afya na lishe.

Na Asha Madohola

Wanufaika wa Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini (TASAF) wilayani Kilosa, wameeleza mafanikio makubwa waliopata kupitia mpango huo wa miaka kumi, huku wakiiomba Serikali kuendeleza msaada huo kutokana na mahitaji yanayoendelea kuwapo kwenye jamii.

Mnufaika wa Tasaf Bw Omary Somvi

Wakizungumza katika Kijiji cha Rudewa kwa nyakati tofauti akiwemo Omary Somvi, wanufaika hao wamesema TASAF imekuwa mkombozi wa maisha yao kwa kuwasaidia kupata chakula, kupeleka watoto shule, kujenga makazi bora na hata kuanzisha biashara ndogondogo.

Sauti ya mnufaika wa Tasaf Omary Somvi
Mnufaika wa Tasaf Bi Sikudhani

Hata hivyo akizungumza mnufaika Sikudhani Kibwana alitoa wito kwa Serikali kuangalia uwezekano wa kuanzisha awamu mpya ya TASAF, wakisema bado kuna makundi mengi yenye uhitaji mkubwa wa msaada na uwezeshaji kwa mustakabali bora wa maisha.

Sauti ya mnufaika Sikudhani
Mwenyekiti Kijiji cha Rudewa Batini Ndg Msabaha

Mwenyekiti wa Kijiji cha Rudewa, Masudi Msabaha, amesema mafanikio ya mradi huo yameonekana wazi kwa wanavijiji, ambapo baadhi yao sasa wana uwezo wa kujitegemea.

Sauti ya Mwenyekiti Masudi Msabaha
Mwezeshaji wa Tasaf Kilosa Bi Mwanaidi Rajabu

Kwa upande wake, Mwezeshaji wa TASAF ngazi ya Wilaya, Bi. Mwanaidi Rajabu, amesema tangu kuanza kwa mpango huo mwaka 2013, kaya zaidi ya 10,000 zimeandikishwa na wanufaika zaidi ya 35,000 wamepata ruzuku pamoja na kushiriki katika vikundi vya kuweka akiba na kuongeza kipato.

Sauti ya Mwezeshaji Bi Mwanaidi

Naye Mratibu wa TASAF wilayani Kilosa, Dedan Maube, amesema malipo yanayoendelea ni ya mwisho kwa awamu hii, na walengwa wamepatiwa bonasi ili kuendeleza shughuli za kiuchumi.

Hata hivyo amewahimiza wanufaika kutumia vizuri fedha hizo kwa maendeleo ya familia na jamii zao.

Sauti ya Mratibu Tasaf Kilosa Ndg Maube

Dirisha la malipo kwa wanufaika wa mradi wa Tasaf kwa siku ya kwanza ambalo limeanza 19 Agosti 2025 limefanyika katika vijiji vya kata za Magomeni, Kasiki, Mkwatani, Chanzuru, Mabwerebwere, Kimamba A&B, Parakuyo, Madoto, Rudewa, na Mvumi.

Mnufaika wa Tasaf akitia saini fomu yake ya malipo