Radio Jamii Kilosa

NMB yatoa msaada wenye thamani ya shilingi milioni 33.1 Kilosa

28 August 2024, 12:59 pm

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Mhe Shaka Hamdu Shaka akipokea madawati kutoka Benki ya NMB. Picha na Kitengo cha mawasiliano serikalini.

Na Asha Madohola

Katika kuunga mkono juhudi za serikali kwenye sekta ya afya na Eeimu, benki ya NMB imetoa msaada wa madawati, meza na vifaa tiba ikiwemo mashine za kupimia mapigo ya moyo, magodoro na Mashuka vyenye thamani ya shilingi milioni 33.1.

Akizungumza baada ya kukabidhiwa Msaada huo Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Mhe. Shaka Hamdu Shaka 27 Agosti, 2024 katika kituo cha afya Kimamba na baadae Shule ya Sekondari Chanzuru amesema Bank ya NMB imekuwa ikishirikiana na Jamii wakati wa changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika wilaya ya Kilosa na kuutaka uongozi na jamii kwa ujumla kuvitunza vifaa hivyo kwa ili vitumike muda mrefu.

Kwa Upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa Ndg. Michael John Gwimile ameishukuru Bank ya NMB kwa msaada huo na kusema kuwa vifaa hivyo vitakwenda kuboresha sekta ya elimu huku akiwataka wanafunzi hususan kidato cha nne kusoma kwa bidii ili kupata ufaulu mzuri katika Mitihani yao ya mwisho.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa Mhe Wilfred Sumari

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri Mhe. Wilfred Sumari alisema Benki ya NMB imekuwa ikijali jamii wakati wa changamoto mbalimbali na kutoa mchango mbalimbali pale inapohitajika kufanya hivyo, Vilevile ameupongeza uongozi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na Ofisi ya Mkurugenzi kwa kusimamia vyema utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Kati Bi Janeth Shango

Kwa upande wake Meneja wa Benki ya NMB kanda ya Kati Bi. Janeth Shango alisema Benki ya NMB hutoa msaada pindi Maafa yanayojitokeza katika maeneo mbalimbali na Kilosa imekabidhi madawati 235 kwa ajili ya shule za Msingi 4 ambazo ni dawaka senta 65, Tindiga 60, Malangari 50, mbigiri 60 pamoja na viti 50 na meza 50 kwa ajili ya shule ya Sekondari Chanzuru sambamba na vifaa tiba magodoro 60, mashuka 60 na mashine za presha 3 vyenye thamani ya shilingi milioni 33. 1 ili kuboresha mazingira bora kwa wananchi.

“Benki ya NMB inayo Sera ya kurejesha kwa jamii faida inayopatikana ili kuboresha mazingira kwa wananchi katika sekta mbalimbali kama vile Elimu, ambapo hutoa madawati kwa shule za msingi, viti na meza kwa shule za Sekondari na vifaa vya kuezeka kwa shule zote sambamba na sekta ya Afya ambapo uchangia vifaa tiba vinavyohitajika katika eneo husika alisema Bi Janeth Shango”.