Radio Kwizera
Radio Kwizera
May 12, 2026, 3:49 pm

Kufikia mafanikio hayo ni juhudi kubwa ambazo wadau wamezifanya ikiwemo halmashauri ya wilaya ya Kibondo, Shirika la UNDP pamoja na shirika la kuhudumia viwanda Vidogo SIDO
Na Samwel Masunzu- Kibondo, KIGOMA
Baadhi ya wafugaji wa samaki wilayani Kibondo mkoani Kigoma wameiomba jamii wilayani humo kuendelea kuthamini na kuunga mkono uwekezaji unaofanywa kwenye maeneo yao ili kukuza uchumi wa wazawa na halmashauri kwa ujumla.
Halmashauri kupitia idara ya maendeleo ya jamii imekuwa ikihamasisha vijana kuunda vikundi na kuanzisha miradi ya maendeleo ili waweze kutambuliwa na kuendelezwa kupitia mikopo ya asilimia 4 kwa vijana, 4 kwa wanawake na 2 kwa watu wenye ulemavu.
Baadhi ya wafugaji wa samaki kutoka kikundi cha Bondeni Fish Farmingi kilichopo Kilemba Kibondo ambao ni Bw. Alex Ntenderi na Bw. Braison Juma wamesema kiu yao ni kuona mazao ya samaki yakiwa utambulisho mkubwa kwa wilaya ya Kibondo kwani samaki wanaofugwa kwenye mabwawa yao hawana utofauti na wanaotoka kwenye maeneo mengine
Bw. Ntenderi anasema hadi kufikia mafanikio hayo ni juhudi kubwa ambazo wadau wamezifanya ikiwemo halmashauri ya wilaya ya Kibondo, Shirika la UNDP pamoja na shirika la kuhudumia viwanda Vidogo SIDO na kwamba bado wanahitaji uungwaji mkono hasa kupata mashine ya kuzalisha vyakula vya samaki inayogharimu zaidi ya shilingi milioni 12.