FM Manyara
FM Manyara
09/03/2026, 21:49

Na Marino Kawishe
Kituo cha taarifa na maarifa kilichopo Kata ya Mamire Wilayani Babati Mkoani Manyara chini ya Mtandao wa Jinsia Tanzania TGNP leo kimeadhimisha siku ya wanawake duniani kwakutoa vitu mbali mbali kwa wanafunzi zaidi ya Ishirini na tano wanaosoma shule ya msingi Samta iliyopo katika kata hiyo.
Akisoma Risala ya siku ya wanawake mbele ya wananchi pamoja na wanafunzi wa shule ya msingi Samta mjumbe wa kikundi Joice Elias amesema changamoto za ukatili kwenye kata hiyo zimeendelea kupungua kwasababu ya juhudi zinafanywa na wana kikundi hicho kwa kushirikiana na jamii inayozunguka eneo hilo.
Naye mgeni Rasmi kwenye maadhimisho hayo afisa maendeleo ya jamii kata ya Mamire Pili Njonju amewataka wanafunzi kutofumbia macho matendo ya kikatili yanayoweza kufanywa kwao kwa kutoa taarifa kwenye vituo vya polisi au kwa wazazi mahiri ambao wamekuwa na mchango kwenye mapambano ya ukatili.
Akishukuru kwa niaba ya wananchi waliojitokeza kwenye sherehe ya maadhimisho ya siku ya Wanawake Diwani wa viti maalumu kata ya Mamire Secilia Edward amewataka wananchi kuchangamkia fursa za mikopo zinazotolewa na serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Suluhu Hassan ili kutatua changamoto kwenye jamii.
Maadhimisho ya siku ya wanawake duniani kwenye kata ya Mamire Wilayani Babati Mkoani Manyara yamefanyika March 9 katika shule ya msingi Samta iliyopo kwenye kijiji cha mwikantsi ambacho kinatajwa kuwa na matukio mengi ya ukatili kwa siku za karibuni na maadhimisho hayo yameandaliwa na kituo cha Taarifa na maarifa kwa ushirikiano na mtandao wa Jinsia Tanzania TGNP.
