FM Manyara

 Manyara kutoa chanjo saratani ya mlango wa kizazi kwa mabinti

April 21, 2024, 12:01 am

Picha ya afisa elimu ya afya kwa umma mkoa wa Manyara akizungumza na Fm Manyara

Serikali  imeanza kampeni ya chanjo ya mlango wa kizazi  kwa mabinti kuanzia umri wa miaka 9 hadi 14 itakayotolewa katika shule za msingi na sekondari pamoja na vyuo ili kuwaepusha   na saratani ya mlango wa kizazi.

Na Hawa Rashid

Zaidi ya mabinti laki moja na nusu  mkoani Manyara wenye umri kuanzia miaka 9 hadi 14  wanatarajiwa kupatiwa chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi  ambayo inatolewa nchi nzima bila malipo ambapo wazazi na walezi  wametakiwa  kuwapeleka watoto wao kwenye vituo vya afya ili kupata njanjo hiyo.  

Akizungumza na FM Manyara,  Afisa elimu ya afya kwa umma mkoa wa Manyara Sweten Mwabulambo amesema  chanjo hiyo ni muhimu kwa mabinti  hao  na  zitatolewa katika shule za msingi na sekondari pamoja na vyuo vyote vilivyopo mkoani hapa ambapo wataalam wa afya watafika katika maeneo hayo ili kutoa chanjo hiyo.

Sauti ya afisa elimu ya afya kwa umma mkoa wa Manyara

Amesema serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeona umuhimu wa kuanzisha chanjo  hiyo kwa lengo la kumkinga binti  asipate saratani ya  shingo ya kizazi ambayo imekuwa ni tatizo kwa akina mama  nchini.

Aidha, amesema miongoni mwa mikoa itakayoadhimisha wiki ya chanjo kitaifa ni mkoa wa Manyara  ambapo shughuli mbalimbali zitafanyika ikiwemo utoaji  wa chanjo za aina tofauti zitakazotolewa kwa mabinti na kilele cha maadhimisho hayo kinatarajiwa kufanyika  mkoani Mwanza. 

Sauti ya afisa elimu ya afya kwa umma mkoa wa Manyara