FM Manyara
FM Manyara
13/03/2026, 21:05

Na George Augustino
Kamati ya kudumu ya Bunge ya maji na mazingira leo imefanya ziara katika Mkoa wa Manyara na kukagua maendeleo ya mradi wa tangi la maji lililopo kata ya Bashay, wilaya ya Mbulu lenye uwezo wa lita millioni mbili yaani Dambia–Haydom wenye thamani ya shilingi bilioni 41.2 fedha kutoka Serikali kuu na wafadhili unaotarajiwa kuhudumia vijiji 21.
Ziara hiyo iliyoongozwa na Mwenyekiti wa kamati ya kudumu ya Bunge ya maji na mazingira, Jackson Kiswaga, akiambatana na wajumbe wa kamati hiyo wakiongozwa na mkuu wa wilaya ya mbulu Michael Semindu ambaye pia alimuwakilisha mkuu wa mkoa wa manyara Queen Sendiga kukagua utekelezaji wa mradi huo muhimu wa maji.

Akizungumza baada ya ukaguzi, Kiswaga ameeleza kuridhishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi huo na ubora wa kazi inayoendelea, ambapo ,ameahidi kuwa kamati ya Bunge itaishauri serikali kuongeza bajeti ya sekta ya maji ili kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi katika maeneo yote ya nchi, huku akiwahimiza wananchi kulinda vyanzo vya maji ili miradi hiyo iwe endelevu.
Kwa upande wake, mkuu wa wilaya ya mbulu, Michael Semindu, ameahidi kuwa uongozi wa wilaya utaendelea kusimamia na kulinda vyanzo vya maji pamoja na miundombinu ya mradi huo ili uweze kudumu na kuwahudumia wananchi kwa muda mrefu.
Nao baadhi ya wananchi wa eneo uliopo mradi pamoja na viongozi wao akiwemo mwenyekiti wa chama cha mapinduzi wilaya ya mbulu wamemshukuru Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania samia suluhu hasan kwa kuwapelekea mradi huo wamaji utakao waondosha katika taabu ya katumia maji machafu.
Mradi wa maji wa dambia–haydom unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi wa vijiji 21 vya wilaya ya mbulu na hivyo kuboresha afya na shughuli za kijamii na kiuchumi katika maeneo hayo.
