FM Manyara
FM Manyara
16 February 2026, 5:16 pm

Shirika la Lesson in Conservation (L.I.C) kwa kushirikiana na Taasisi ya Chem Chem Association wamezindua mradi wa elimu ya uhifadhi mashuleni unaolenga shule za msingi na sekondari zilizopo katika kata tatu zinazunguka hifadhi ya Tarangire na Manyara.
Na Marino Kawishe
Akizungumza na maafisa elimu kata na wakuu wa idara mbali mbali kutoka halmashauri ya wilaya ya Babati mwakilishi wa shirika hilo GloriaTarimo amesema mradi huo utawafikia jumla ya watoto elfu tano kutoka shule za msingi na sekondari zitakazofikia 21, kutoka kata ya Nkaiti, Mwada na Magara ambao utatekelezwa kwa miaka mitano.
Kwa upande wake mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Babati Anna Mbogo amesema mradi huo unapaswa kutoa elimu kwa wanafunzi wa shule hizo kwa manufaa ya kizazi cha leo na baadae huku akizitaka idara za elimu na mali asili kuingiza kwenye mipango yao masuala yanayohusu uhifadhi.
Nae mkurugenzi mtendaji wa Taasisi ya Chem Chem Association Clever Zulu amesema lengo la Taasisi hiyo ni kujenga jumuiya ya mfano Africa kupitia uhifadhi wa jamii chini ya jumuiya ya Burunge WMA na wananchi kwenda kujifunza namna bora ya uhifadhi kwenye maeneo yao.
Aidha,mradi huo pamoja na mambo mengine utawapa fursa wanafunzi kutembelea maeneo ya hifadhi hapa nchini na kujifunza kwa vitendo faida za uhifadhi na ukitarajiwa kugharimu zaidi ya shilingi milioni 156 mpaka kukamilika kwake.