FM Manyara
FM Manyara
10 January 2026, 12:57 pm

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray, ametoa wito kwa Waajiri kote nchini kuhakikisha maadili, kanuni na haki za Watumishi wa Umma vinatekelezwa kwa ufanisi ili kuboresha huduma kwa wananchi na kuongeza tija kazini.
Na Mzidalfa Zaid
Mhe. Qwaray ameyasema hayo akiwa katika ziara yake Wilayani Babati, Mkoa wa Manyara, ambapo alizungumza na watumishi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Taasisi mbalimbali, pamoja na Halmashauri ya Mji wa Babati na Halmashauri ya Wilaya ya Babati kwa nyakati tofauti.
Amesisitiza umuhimu wa ushirikiano, uzalendo na kufanya kazi kwa bidii, huku akiagiza waajiri kuhakikisha waajiriwa wapya wanapatiwa mafunzo ndani ya miezi mitatu baada ya kuajiriwa ili kuongeza ufanisi. Vilevile, ameelekeza kuwa waliostahili kuthibitishwa kazini wafanyiwe hivyo haraka ili kuepusha kukaimu kwa muda mrefu.
Aidha, amewataka waajiri kushughulikia changamoto za watumishi ndani ya siku tatu na kutoa mrejesho kwa wakati, sambamba na kuhakikisha haki na stahiki zao zinalipwa kwa wakati.