FM Manyara

Serikali yalipa fidia bilioni 2.9 Manyara

24 October 2025, 8:47 pm

Mkuu wa mkoa wa Manyara Queen Sendiga pamoja na mkuu wa wilaya ya Babati Emmanuela Kaganda. Picha na Mwandishi wetu.

Kaya (28) za maeneo ya Msasani Maisaka A na Maisaka Kati Wilayani Babati, mkoa wa Manyara zimelipwa fidia ya bilioni 2.9 baada ya maeneo yao kuchukuliwa  na serikali kwa matumizi ya huduma za kijamii.

Na Mzidalfa Zaid

Taarifa ya malipo ya fidia hiyo zimetolewa na Mkuu wa mkoa wa Manyara Queen Sendiga kupitia kikao kilichofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, ambapo amewashukuru na kuwapongeza wananchi hao kwa kuridhia kuyaachia maeneo hayo ya vyanzo vya maji kwa manufaa ya jamii nzima ya wakazi wa Wilaya ya Babati ambao hutegemea chanzo hicho. 

Amewataka wananchi hao kuridhika na kiwango kilichotolewa na serikali Baada ya kufanyika kwa tathmini ya mwisho mwaka 2024 huku akiwaahidi kuwapatia viwanja vya bei nafuu vilivyopimwa na kuwasihi wananchi hao kutumia fedha hizo za fidia kujenga makazi mapya na kujiendeleza kiuchumi.

Sauti ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara Queen Sendiga

Aidha, baadhi ya wananchi hao Kupitia kikao hicho wamemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Manyara Queen Sendiaga kwa kufuatilia na kusimamia kwa ukaribu malipo ya fidia ya maeneo yao .

Wamesema kuwa wamekaa muda mrefu tangu mwaka 2008 pasipo kujua hatma yao ambapo wameushukuru uongozi wa Serikali ya awamu ya sita kwa kuweza kukata kiu yao ya muda mrefu.

Sauti ya wananchi

Aidha, Sendiga ametoa muda wa miezi sita kwa  wananchi hao kuondoka kwa hiari kwenye maeneo hayo ili Mamlaka ya Maji Babati (BAWASA) waanze kutekeleza mradi mkubwa wa usambazaji wa maji katika Mji wa Babati.