Serikali Kasulu yasisitiza leseni za kufungisha ndoa
Buha FM Radio

Serikali Kasulu yasisitiza leseni za kufungisha ndoa

28 July 2026, 11:50 am

Katibu Tawala wa Wilaya ya Kasulu, Bi. Theresia Mtewele, wakati wa hafla ya kumsimika Askofu wa Jimbo la Kigoma kupitia Kanisa la Hope For All Nations (HOFAN). Picha na Paulina Majaliwa.

Kutokana na changamoto ya migogoro ya ndoa na ndoa nyingi kuvunjika,viongozi wa Madhehebu mbaalimbali wilayani Kasulu wameombwa kusimami kwa ukamilifu zoezi la ufungishaji wa ndoa, wakitakiwa kuwa na leseni au bibali vya ufungishaji wa ndoa.

Na; Paulina Majaliwa

Serikali imewataka viongozi wa makanisa wilayani Kasulu mkoani Kigoma kuhakikisha wachungaji wanaofungisha ndoa wanakuwa na vibali au leseni halali na zilizo hai, hatua itakayorahisisha utatuzi wa migogoro ya ndoa pamoja na kulinda uhalali wa ndoa zinazofungwa nchini.

Wito huo umetolewa na Katibu Tawala wa Wilaya ya Kasulu, Bi. Theresia Mtewele, wakati wa hafla ya kumsimika Askofu wa Jimbo la Kigoma kupitia Kanisa la Hope For All Nations (HOFAN), iliyofanyika katika Halmashauri ya Mji Kasulu ambapo amesema ndoa zinazofungishwa na viongozi wenye leseni halali hurahisisha kazi ya Msajili wa Ndoa na vyombo vya serikali kushughulikia migogoro ya kifamilia, hali inayoweza kupunguza ongezeko la watoto wanaoishi mitaani.

Sauti ya Bi. Theresia Mtewele.

Aidha, Bi. Mtewele amewataka viongozi wa dini kushirikiana na waumini pamoja na jamii kuwaandaa vijana kwa misingi bora ya ndoa na maadili, ili kupunguza kasi ya kuvunjika kwa ndoa kunakotokana na sababu zisizo za msingi.

Sauti ya Bi. Theresia Mtewele.

Kwa upande wake, Kiongozi Mkuu na mwanzilishi wa Kanisa la Hope For All Nations (HOFAN), Askofu Dkt. Charles Jangalason, amesema umoja na mshikamano ni msingi muhimu wa maendeleo ya taifa na kuwataka viongozi wa kanisa hilo kuwafundisha waumini misingi ya imani ya kweli ili kuepusha taharuki, migawanyiko na migogoro ndani ya kanisa na katika jamii kwa ujumla.

Sauti ya Askofu Dkt. Charles Jangalason.
Kiongozi Mkuu na mwanzilishi wa Kanisa la Hope For All Nations (HOFAN), Askofu Dkt. Charles Jangalason. Picha na Paulina Majaliwa.

Naye Askofu mteule wa Jimbo la Kigoma, Askofu Alex Kalalaye, amewashukuru viongozi na waumini wa kanisa hilo kwa kumuamini na kumpa jukumu la kuliongoza jimbo hilo pamoja na kutoa ahidi ya kushirikiana kwa karibu na Serikali ya Wilaya ya Kasulu katika kudumisha amani, umoja na maendeleo ya jamii.

Sauti ya Askofu mteule wa Jimbo la Kigoma, Askofu Alex Kalalaye.
Picha ya pamoja baada ya zoezi la kumsimika Askofu mteule wa Jimbo la Kigoma, Askofu Alex Kalalaye, mwenye vazi la langi ya zambalau katika akiwa na viongozi wengine wa Dini na Serikali. Picha na Paulina Majaliwa.