Buha FM Radio
Buha FM Radio
17 April 2026, 5:06 pm

“Lengo la hospitali yetu ni kuwasaidia wagonjwa kwa ukaribu zaidi kama sera ya wizara ya afya inavyotaka hivyo hata sisi tumesogeza huduma hizi za kibingwa ili kurejesha matumaini ya wananchi wa Kasulu na maeneo mengine jirani” Amesema Dkt. Kitenyi.
Na; Sharifat Shinji
Zaidi ya wananchi 500 wa Wilaya ya Kasulu na Mkoa wa Kigoma kwa ujumla wamenufaika na huduma ya Kambi ya madaktari bingwa inayoendelea katika hospitali ya Rufaa Kabanga iliyopo wilayani Kasulu katika Mkoa wa Kigoma.
Hayo yameelezwa na Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo Dkt. Peter Kitenyi wakati akieleza jinsi zoezi la utowaji huduma kwa wananchi, ambapo amesema mwitikio wa wananchi kufika katika hospitali hiyo ni mkubwa huku akitaja zaidi ya wananchi 500 wameshapata huduma ya kuonana na madakitari hao.
Aidha Dkt. Kitenyi ameeleza huduma mbalimbali zinazotolewa katika kambi hiyo ya madaktari bingwa ambapo amesema lengo nikuwahudumia wananchi wa Wilaya ya Kasulu kwa ukaribu zaidi huku akitoa pongezi kwa wafanyakazi wote wa hospitali hiyo.

Kwa upande wake Evarist Mwelongo ambaye amezungumza kwa niaba ya wagonjwa wengine amesifia huduma aliyoipata kutoka kwa madakitari bingwa wa meno huku akiwasisitiza wananchi wengine kutumia furusa ya Kambi hiyo kufanya vipimo vya uchunguzi wa afya zao.
Hospitali ya Rufaa Kabanga imekuwa na utaratibu wa kuendesha kambi za madakitari bingwa kila mwezi ikiwa mwezi huu kambi hiyo imeanza April 13 hadi April 17 huku zaidi ya wananchi 500 wakiwa wamefika kupata huduma katika hospitali hiyo.
