Madiwani Kasulu wasisitizwa kusimamia miradi ya maendeleo
Buha FM Radio

Madiwani Kasulu wasisitizwa kusimamia miradi ya maendeleo

29 July 2026, 6:58 pm

Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu wakiwa katika ukumbi wa Halmashauri wa Kagoma. Picha na Ramadhan Zaidy.

Kufuatia kuanza kwa mwaka mpya wa fedha, Mkuu wa Wilaya ya Kasulu amewataka watumishi na viongozi kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uwajibikaji na ushirikiano ili kuhakikisha vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Sita vinatekelezwa kwa ufanisi.

Na; Ramadhan Zaidy

Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma wametakiwa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uwajibikaji na ushirikiano ili kuhakikisha vipaumbele vya Serikali vinatekelezwa kwa ufanisi na kuwanufaisha wananchi.

Wito huo umetolewa na Katibu Tawala wa Wilaya ya Kasulu, Bi. Theresia Mtewele, aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya katika kikao cha robo ya nne cha Baraza la Madiwani la Halmashauri hiyo. Amesema ni muhimu kwa kila diwani kuhakikisha anatoa mrejesho kwa wananchi kuhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika maeneo anayoyawakilisha.

Sauti ya Bi. Theresia Mtewele.
Katibu Tawala wa Wilaya ya Kasulu, Bi. Theresia Mtewele akitoa salamu za Mkuu wa Wilaya Mhe. Kanali Isac Mwakisu kwa Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu. Picha na Ramadhan Zaidy.

Naye Mbunge wa Jimbo la Kasulu Vijijini, Edibily Kazala, amewashukuru madiwani kwa ushirikiano wanaoendelea kumpa katika kusimamia na kutekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo ndani ya jimbo hilo.

Sauti ya Mbunge wa Jimbo la Kasulu Vijijini, Edibily Kazala.

Kwa upande wao, baadhi ya madiwani wa Halmashauri hiyo wamesema fedha zilizotengwa na Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/2027 zimeanza kufika katika maeneo yao, hatua ambayo itasaidia kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi.

Sauti za madiwani.
Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu, Charles Benjamini, ambaye ndiye aliyeendesha Kikao cha Robo ya Nne cha Baraza la Madiwani la Halmashauri hiyo. Picha na Ramadhan Zaidy.

Akiwasilisha salamu za Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Kasulu ameliagiza Baraza la Madiwani kuhakikisha changamoto zote zilizowasilishwa katika kikao hicho zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati, ili kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa miradi na kuboresha huduma kwa wananchi.

Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu wakiwa katika ukumbi wa Halmashauri wa Kagoma. Picha na Ramadhan Zaidy.