Mufindi FM
Mufindi FM
3 February 2026, 11:50

“Ndugu zangu viongozi turudi katika miongozo ya chama inavyotuongozo ikiwemo kuvaa sare za chama, kuitisha vikao na mikutano“ Bi. Mkini
Na Marko Msafiri.
Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi (UWT) wilaya ya Mufindi, imewataka viongozi wa jumuiya hiyo kurudi katika kanuni za chama zinazowaongoza wanachama katika shughuli mbalimbali za kichama ikiwemo kuitisha mikutano na vikao.
Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa jumuiya hiyo, Marcelina Mkini, katika maadhimisho wa miaka 49 tangu kuasisiwa kwa chama hicho cha Mapinduzi (CCM) yaliyofanyika kiwilaya katika uwanja wa Mashujaa mjini Mafinga.
Maadhimisho hayo yametanguliwa na matendo ya huruma katika Hospitali ya Mji Mafinga kwa jumuiya hiyo ya umoja wa wanawake kutembelea hodi ya wazazi na kutoa msaada.
Baada ya kukabidhi msaada huo, Elizabethi Kilenyi ambaye ni miongoni mwa wanufaika, ameipongeza jumuiya hiyo na kuwataka waendelee na moyo huo wa majitoleo.
Bi. Rehema Mbedule ambaye ni Mjumbe wa kamati ya utekelezaji wilaya na mshiriki katika maadhimisho hayo, amesema kama wanawake wakihamasika, watazingatia malezi na kuwaepusha vijana wasiingie katika uvunjifu wa amani.

Maadhimisho hayo ya miaka 49 ya Chama cha Mapinduzi (CCM) yamebeba ujumbe usemao “Umoja na Amani kwa maendeleo ya Taifa Letu”.