Mufindi FM
Mufindi FM
3 February 2026, 10:43

“Viuatilifu ni sumu, vinapaswa vitumike kwa uangalifu” Mtoka
Na Jackson Machowa.
Wakulima Nyanda za Juu Kusini wametakiwa kuzingatia matumizi sahihi ya viuatilifu katika kipindi chote cha kilimo ili kujihakikishia wingi na ubora wa mazao shambani.
Wito huo umetolewa kufuatia shughuli za uzalishaji wa mazao ya kilimo kukabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo magugu na wadudu waharibifu na hivyo kumlazimu mkulima kutumia viuatilifu ili kukabiliana na hali hiyo.
Bwana Ezekiel Mtoka ni  mtaalam wa kilimo kutoka shirika la Nafaka Kilimo linalotekeleza mradi wa Farm to Maket Allience chini ya ufadhili wa shirika la mpango wa chakula duniani (WFP) amewataka wakulima kutambua hatari ya viuatilifu kwa afya ya binadamu na jamii kwa ujumla ikiwa havitatumika kwa uangalifu.
Hayo yanajiri katika mafunzo ya siku moja yaliyowakutanisha wadau wa makundi mbalimbali ya mnyororo wa thamani wa kilimo kutoka Halmashauri za Mufindi, Njombe na Wanging’ombe yaliyofanyika mjini Makambako yakiwa na lengo la kuongeza uelewa wa namna sahihi ya kukabilana na visumbufu mashambani.
Bwana Moses Logan ambaye ni Mratibu wa mradi wa Farm to Market Allience amesema mradi huo unawanufaisha wakulima kwa kupata elimu ya kilimo bora na kuunganishwa na masoko kupitia watoa huduma au vituo vya huduma 320 vilivyopo katika mikoa ya Iringa, Njombe na Mbeya.
Maofisa wa serikali wanaohudumu katika idara za kilimo akiwemo Bw. Paul Year ni miongoni mwa waalikwa wa mafunzo hayo ambaye ametoa rai kwa wakulima kuwatumia vyema maafisa ugani ili kuzitekeleza mbinu za kilimo bora huku washiriki wenyewe akiahidi mabadiriko ili kufanikisha malengo ya kiuchumi na kijamii ya mkulima mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.