Radio Fadhila

Mtoto achomwa mikono kisa korosho

14 November 2025, 10:13 AM

Picha kwa msaada wa mtandao

“Mtuhumiwa huyu ambaye ni Katibu wa UVCCM kata ya Namalenga licha ya kumchoma moto mtoto wake wa kambo, lakini pia amemuadhibu vibaya mtoto mwingine ambaye alishirikiana nae wakati wa kuuza korosho”

Na Neema Nandonde

Salumu Hussein Maona  mkazi  wa kitongoji cha Temeke Mkangaula  ambaye pia ni Katibu wa Vijana CCM kata ya Namalenga wilayani Masasi Mkoani Mtwara, amemchoma moto maeneo ya mikononi mtoto wake wa  kambo  Abdul Zahoro Paulo (11) mwanafunzi wa darasa  la  nne,  baada  ya  kuiba korosho.

Akizungumza  na  redio Fadhila, Mwenyekiti  wa  kitongoji hicho Ismail Shaibu, amesema tukio hilo limetokea novemba 12, 2025 ambapo wazazi wa mtoto huyo waliondoka nyumbani na kumuacha mtoto huyo akiwa  na  watoto  wenzake.

Baada ya baba kurejea, akagundua walipohifadhi korosho zimepungua, na alipofuatilia akabaini kuwa Abdul amechukua takribani kilo 3 na kwenda kuziuza kwa mnunuzi asiye rasmi kwa shillingi 4500.

Kufuatia hilo, Mtuhumiwa akafunga mikono ya mtoto huyo kwa kamba, na kufungua koki ya pikipiki yake kisha akamwagia petroli mikono hiyo ndipo alipompeleka ndani na kumchoma moto.

Sauti ya Mwenyekiti  wa  kitongoji cha Temeke Mkangaula Ismail Shaibu

Kwa upande wa  majirani  na  mashuhuda  wa tukio hilo, wameeleza kuwa baba huyo ni kawaida kumfanyia  matukio ya  ukatili mtoto huyo, lakini mengi yamefichwa na mama  yake na hili limethibitika kwakuwa ni kubwa zaidi.

Sauti ya mashuhuda na ndugu wa mtoto

Naye baba aliyefanya  tukio hilo la kikatili, amekiri kutenda kosa hilo huku akijutia  kuwa  haikuwa adhabu nzuri kwa  mtoto.

Sauti ya Mtuhumiwa Salumu Hussein Maona

Kwa mujibu wa mwenyekiti wa kitongoji cha Temeke Mkangaula,  ameeleza  kuwa taratibu nyingine za kisheria zimeanza kuchukuliwa ili kuhakikisha  kuwa baba huyo anaadhibiwa kwa mujibu wa sheria.