Radio Fadhila

Wananchi acheni kupuuzia maelekezo yanayohusu usafi wa mazingira-Ame

19 September 2025, 12:43 PM

Afisa Afya Mazingira Halmashauri ya Wilaya Masasi, Said Ame wakati anazungumza na wananchi kuhusu siku ya usafi duniani kupitia redio Fadhila. Picha na Neema Nandonde

Wakati mwingine wananchi hususani wanaoishi vijijini wanaishi kwa mazoea, kama mtu amezaliwa na kukulia kwenye nyumba isiyo na shimo la taka na yeye analazimisha aishi hivyo siku zote

Na Neema Nandonde

Kuelekea maadhimisho ya siku ya usafi duniani ambayo hufanyika kila ifikapo septemba 20, wananchi wa halmashauri ya wilaya Masasi mkoani Mtwara wametakiwa kuacha kupuuzia maelekezo ya usafi wa mazingira yanayotolewa na wataalam, ili kuondoa athari zitokanazo na mazingira machafu.

Hayo yameelezwa septemba 19, 2025 na Afisa Afya Mazingira Halmashauri ya Wilaya Masasi, Said Ame alipokuwa anazungumzia siku ya usafi duniani kwenye kipindi cha Fadhila Mseto kinachorushwa na redio Fadhila.

Sauti ya Afisa Afya Mazingira Halmashauri ya Wilaya Masasi, Said Ame

Kwa upande wake Afisa Afya Mazingira Halmashauri ya wilaya Masasi, Glory Masawe amezungumzia  kaulimbiu  ya  siku ya  usafi duniani kwa mwaka  2025 ambayo inasema “Tunza mazingira kwa kuzipa taka thamani” ambapo amefafanua  kuwa  si kila  taka inatupwa moja kwa moja, bali zipo taka ambazo zinaweza kutumika tena baada ya kuziongezea thamani  kwa  kuzirejeleza au kubadilishia matumizi.

Sambamba  na  hilo amewataka baadhi  ya  wafanyabiashara  kuacha tabia ya   kutii amri ya  kufunga maeneo ya biashara  kwa muda kwenye siku maalumu za usafi,  akiwasisitiza  kushiriki  kufanya  usafi  na  si kubaki nyumbani na kusubiri muda wa kufungua  maeneo hayo.

Maafisa Afya Mazingira Halmashauri ya Wilaya Masasi, Said Ame na Glory Masawe wakati wanazungumza na wananchi kuhusu siku ya usafi duniani kupitia redio Fadhila. Picha na Neema Nandonde

Halmashauri ya wilaya Masasi, inatarajia kuadhimisha siku ya usafi duniani katika kata ya Ndanda ambapo baadhi ya watumishi wa serikali, wananchi na taasisi zisizo za kiserikali watakutana kwa lengo la kufanya usafi wa mazingira kwa pamoja, huku wananchi wengine wakisisitizwa kufanya usafi kwenye maeneo yanayowazunguka.