Radio Fadhila

Kumnywesha maji  mtoto aliye chini ya miezi 6 kunaharibu mfumo wa chakula

5 August 2025, 3:30 PM

Afisa Lishe wa Halmashauri ya mji Masasi Omari Mushi akiwa anatoa elimu ya unyonyeshaji kupitia redio Fadhila. Picha na Godbless Lucius

“Jamii  iache  kuishi  kwa  mazoea kwenye  suala  la   malezi hususani unyonyeshaji  wa maziwa  ya  mama ili  kuwaandaa  watoto  wenye  ukuaji  bora  kimwili  na  kiakili”

Na Neema Nandonde

Kufuatia  maadhimisho  ya  wiki  ya unyonyeshaji duniani, jamii wilayani Masasi  mkoani Mtwara, imeaswa kuzingatia  unyonyeshaji sahihi  wa  maziwa  ya  mama pekee ili mtoto  asipatiwe  kinywaji  au  chakula  chochote kabla  ya  kutimiza  miezi 6.

Hayo  yameelezwa  Agosti 5, 2025 na  Afisa  Lishe wa Halmashauri ya  Mji  Masasi  Omari Mushi,  alipokuwa  akizungumza  katika  kipindi  cha  Morning Booster kinachorushwa  na  redio Fadhila.

Amesema  kuwa mtoto mwenye umri  wa  chini  ya miezi  6, anapopewa chakula  au kinywaji tofauti na  maziwa  ya  mama, inasababisha  michubuko  kwenye mfumo wa  chakula, jambo ambalo ni hatari kwa ukuaji wa mtoto.

Sauti ya Afisa  Lishe wa Halmashauri ya  Mji  Masasi  Omari Mushi

Sambamba  na  hayo, Mushi  amefafanua  kuwa  kunyonyesha  hakuharibu  umbo  la  titi  la  mama, bali  mama  akinyonyesha  kwa  usahihi inamsaidia  kuepuka  saratani  ya  matiti  na msongo  wa  mawazo.

Sauti ya Afisa Lishe wa Halmashauri ya Mji Masasi Omari Mushi
Afisa Lishe wa Halmashauri ya Mji Masasi Omari Mushi

Maadhimisho  ya wiki  ya  Unyonyeshaji  ilianza  rasmi  Agosti 1, 2025  na  kilele  chake kitakuwa Agosti 7, 2025  huku kaulimbiu ikisema  kuwa “Thamini Unyonyeshaji weka  mazingira  wezeshi  kwa mama  na  mtoto”