Radio Fadhila

MAMCU yaongoza njia kupambania ushirika kwa vitendo

26 June 2025, 11:19 AM

Picha na MAMCU

“Mnaweza kusafisha ufuta vizuri na mkaufunga kwenye vifungashio, lakini watu wasio waaminifu wakaenda mbele wakabadilisha  vifungashio wakaweka uchafu, MAMCU tutalidhibiti hilo kwa kuzalisha vifungashio vyetu vitakavyohifadhi mazao moja kwa moja”

Na Neema Nandonde

Chama  kikuu cha  Ushirika MAMCU kinachohudumia wakulima wa wilaya ya Masasi, Nanyumbu na Mtwara  mkoani Mtwara, kimedhamiria kuanzisha miradi mbalimbali itakayosimamiwa na chama hicho, ili kuondoa kero zinazowakabili wakulima wanaohudumiwa  na  chama  hicho.

Hayo yameelezwa juni 26, 2025 na Mwenyekiti wa Chama hicho, Alhaji Azam Mfaume, alipokuwa anazungumza kwenye kipindi cha Morning Booster kinachorushwa na redio Fadhila, ambapo amesema miradi hiyo ni ujenzi wa maghala mawili ya kukusanyia mazao wilayani Mtwara, kiwanda  cha  kutengeneza vifungashio  na  kusafishia ufuta wilayani Masasi, kituo cha kisasa cha malipo wilayani Nanyumbu na ununuzi  wa malori  kwaajili ya kusafirishia mazao ya wakulima.

Sauti ya Mwenyekiti wa MAMCU Alhaji Azam Mfaume.
Mwenyekiti wa MAMCU Alhaji Azam Mfaume akiwa redio Fadhila. Picha na Godbless Lucius

Akizungumzia kushuka kwa bei ya ufuta kwa msimu unaoendelea ukilinganisha na msimu uliopita, Alhaji  Mfaume ameeleza kuwa kama  ilivyo biashara  za  kawaida,  kuna kupanda na kushuka na  kwa  msimu  huu kutokana  na  uzalishaji mkubwa  wa  ufuta nchini China ambao ni watumiaji wakubwa  wa  zao  hilo,  kumesababisha kushuka kwa bei  kwa wazalishaji kutoka nchi nyingine  kwakuwa uhitaji ni mdogo nchini humo.

Aidha amewasisitiza  wakulima  kuelekea  msimu  mpya wa  korosho, kuhakikisha wanafuata  ushauri wa wataalam kuhusu matumizi sahihi ya viautilifu.

Sauti ya Mwenyekiti wa MAMCU Alhaji Azam Mfaume

Sambamba  na  hayo, Alhaji Mfaume amewasisitiza  wakulima  kutoa  taarifa sahihi wakati wa  kujisajili kwenye njia mbalimbali  za malipo ili kuondoa  changamoto  zinazojitokeza  wakati wa malipo  baada  ya  kuuza  mazao  yao, ambapo amesema  kwa  msimu huu changamoto hizo kwa  chama cha MAMCU zimepungua  kwa kiasi kikubwa na wakulima wa ufuta wameanza kulipwa fedha zao kwa wakati.