Radio Fadhila

MANAWASA yakaribia kupata ufumbuzi kero mgao wa maji Masasi

23 June 2025, 4:09 PM

Koki inayotoa maji, tayari kwa matumizi ya wateja. Picha na Neema Nandonde

Kutokana  na  ongezeko  la  wateja  wanaohitaji  huduma ya  maji kupitia MANAWASA, kumesababisha  chanzo chetu kuzidiwa  hivyo  kulazimika  kuwa  na  mgao  wa  maji ili kila  mteja  asikose  kabisa maji

Na Neema Nandonde

Mamlaka ya  maji safi  na usafi  wa  mazingira Masasi-Nachingwea (MANAWASA) inayohudumia  wilaya  za  Masasi, Nachingwea, Nanyumbu na baadhi ya  maeneo  ya wilaya  ya  Ruangwa  imeeleza  kuwa, inaendelea  kuibua na kutafiti  vyanzo  mbalimbali vya  maji  na  kuvifanyia  kazi, ikiwemo chanzo  cha  mto Ruvuma,  ili kuhakikisha  kuwa  wananchi wanaohudumiwa na mamlaka hiyo  wanapata  huduma  ya  maji  kila  wakati.

Hayo  yameelezwa  Juni 23, 2025 na  Mkurugenzi wa Usambazaji  Maji MANAWASA  Mhandisi  Aneth Mawenya, alipokuwa  akizungumza   kwenye  kipindi  cha  Morning Booster kinachorushwa  na  redio Fadhila, ambapo amesema kuanzishwa kwa vyanzo hivyo pindi vitakapokamilika kulingana na bajeti ya serikali kutasaidia kuondoa mgao wa maji katika maeneo wanayoyahudumia.

Sauti ya Mkurugenzi wa Usambazaji  Maji MANAWASA  Mhandisi  Aneth Mawenya.
Mkurugenzi wa Usambazaji  Maji MANAWASA  Mhandisi  Aneth Mawenya. Picha na Godbless Lucius

Kwa upande  wake  Mkurugenzi  wa  Huduma kwa  Wateja  MANAWASA  Obadia  Mtuya, amekiri  kuwepo  kwa  changamoto  ya  kucheleshwa  kwa  maunganisho  ya  maji  kwa  wateja  wapya  kwa  miezi michache iliyopita,  huku  kieleza  kuwa  sababu kubwa  ilikuwa  ni uchache wa  mita, lakini hivi  sasa vifaa vimeshafika  na  wateja  wataunganishiwa  huduma  ya  maji  kwa  wakati.

Aidha Mtuya amewataka  wateja  kulipa  ankara  za  maji kwa  wakati,  ili kuondoa  usumbufu  wa kukumbushwa  mara  kwa  mara  na  kuiwezesha mamlaka  hiyo kuendesha  shughuli  zake  ambazo zitarahisisha upatikanaji wa maji  safi na salama  kwa wananchi.

Sauti ya Mkurugenzi  wa  Huduma kwa  Wateja  MANAWASA  Obadia  Mtuya
Mkurugenzi  wa  Huduma kwa  Wateja  MANAWASA  Obadia  Mtuya. Picha na Godbless Lucius

Mamlaka ya maji safi na usafi wa Mazingira Masasi -Nachingwea (MANAWASA), toka kuanzishwa kwakwe imekuwa na ongezeko kubwa la wateja ambapo mwaka 2013 ilikuwa na wateja 3000, na mwaka 2025 wateja wameongezeka hadi kufikia 17,000, jambo linalosabisha chanzo kimoja cha maji kushindwa kutosheleza hivyo kusababisha mgao wa maji kwa wateja.