Radio Fadhila

Usiri watajwa chanzo ukatili kwa watoto Masasi

19 June 2025, 9:37 AM

Mtoto aliyefanyiwa ukatili wa kimwili. Picha na Google

Familia nyingi zinaamua kukaa  kimya pindi  mwanafamilia  anapomfanyia  ukatili  mtoto aliyeko ndani ya  familia  hiyo, kwa kuhofia  kuwa wakiripoti tukio hilo mwanafamilia huyo atachukuliwa hatua

Na Neema Nandonde

Jamii wilayani  Masasi  mkoani Mtwara  imetakiwa  kuacha  kuficha  matukio ya  ukatili dhidi ya  watoto,  ili kukomesha matukio hayo.

Akizungumza  katika  mahojiano maalumu kuhusu siku ya  mtoto wa Afrika juni 16, 2025  yaliyofanyika katika kipindi cha Morning Booster kinachorushwa na  redio Fadhila, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya  Mwanzo Lisekese Zainabu Mtoro, ameeleza  kuwa baadhi ya  familia  zinaficha  matukio ya  ukatili wanayofanyiwa watoto kwakuwa yamefanywa na wanafamilia.

Amesema  kuwa, uwepo wa  usiri huo unasababisha  kutopatikana  ushahidi  wa kutosha kwa baadhi ya kesi zinazohusisha ukatili kwa watoto, jambo linaloifanya jamii iendelee kufanya matukio hayo kwa kuamini kuwa  watayamaliza  wenyewe kwa wenyewe, pasi na sheria kuchukua mkondo wake.

Sauti ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya  Mwanzo Lisekese Zainabu Mtoro
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya  Mwanzo Lisekese Zainabu Mtoro. Picha na Godbless Lucius

Kwa upande wake Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Mwanzo Lisekese Lightness Masimba, ameitaka  jamii  kuachana  na  mila  potofu zinazosababisha  kuleta  ubaguzi kwa  baadhi ya  watoto, jambo linalosababisha  watoto kunyimwa haki zao za msingi.

Sauti ya Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Mwanzo Lisekese Lightness Masimba
Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Mwanzo Lisekese Lightness Masimba. Picha na Godbless

Ikumbukwe kuwa siku ya mtoto wa Afrika, ilitokana na mauaji ya halaiki dhidi ya watoto yaliyofanyika nchini Afrika kusini katika eneo la mji wa Soweto Juni 16 1976, ambapo watoto wengi waliuwawa wakati wa kudai haki zao ikiwemo elimu kutoka kwa makabulu.