Radio Fadhila

Masasi yaandika historia taka ngumu zikigeuzwa fursa

5 June 2025, 7:28 PM

Kituo cha utoaji elimu ya mazingira wilayani Masasi. Picha na Godbless Lucius

Taka zinazozalishwa majumbani na viwandani, bado ni fursa kwa jamii, badala  ya  kuzitupa mtaani wanaweza kutengeneza  mkaa mbadala ambao ni mzuri kwa afya ya  binaadam na mazingira.

Na Neema Nandonde

Kutokana na kuanzishwa kwa kituo cha elimu ya  mazingira kilichopo wilayani Masasi mkoani Mtwara, jamii  wilayani  humo inapata nafasi  kubwa ya kujifunza  kwa  vitendo  kuhusu utunzaji wa mazingira na fursa zake ikiwemo kuzigeuza taka ngumu kuwa na thamani zaidi.

Akizungumza na  redio Fadhila  Juni 5, 2025 kuhusu siku ya mazingira  duniani, Afisa  Mazingira  wa  Halmashauri ya  Mji Masasi Julius Mwikaragate  amesema  kuwa,  kupitia  kituo  hicho cha  elimu ya  mazingira kinasaidia  jamii kugeuza  taka  ngumu  na kutengeneza  vitu mbalimbali ikiwemo nishati safi ya  kupikia (mkaa mbadala).

Aidha  ameeleza  kuwa, kupitia  kituo  hicho  cha  elimu ya  mazingira wataalam wanatoa  elimu ya  umeme  jua, uhifadhi wa misitu, uvunaji wa  maji ya  mvua na  mbinu mbali za uhifadhi wa mazingira  bila malipo yoyote  ili  kuisaidia  jamii  kushiriki kikamilifu katika  utunzaji wa  mazingira  na  kuona fursa zinazopatikana kupitia maliasili mbalimbali  zilizopo kwenye mazingira wanayoishi.

Sauti ya Afisa  Mazingira  wa  Halmashauri ya  Mji Masasi Julius Mwikaragate
Afisa  Mazingira  wa  Halmashauri ya  Mji Masasi Julius Mwikaragate, akiwa ameshika bango linaloonesha miongoni mwa elimu zinazotolewa. Picha na Godbless Lucius

Akizungumzia  kuhusu msisitizo uliowekwa  kwenye  kaulimbiu  ya  siku ya  mazingira  duniani kwa  mwaka 2025 inayosema “Mazingira yetu na Tanzania ijayo; Tuwajibike sasa, dhibiti matumizi ya plastiki”,  Mwikaragate ameeleza athari zinazopatikana  kutokana  na  taka  za  plastiki huku akiitaka  jamii  kudhibiti  taka  hizo.

Sauti ya Afisa  Mazingira  wa  Halmashauri ya  Mji Masasi Julius Mwikaragate

Kituo cha  Elimu ya  mazingira  kwa  vitendo kilichopo wilayani  Masasi mkoani Mtwara,  kimeanzishwa  kwa  lengo la  kuiwezesha  jamii kufahamu athari  za uharibifu wa  mazingira, na namna ya  kuhifadhi  mazingira  ili kuzifikia  fursa zilizopo kwenye maeneo  yao,  kupitia  uwezeshwaji wa miradi mbalimbali unaotolewa na kituo hicho kwa wananchi.

Majiko banifu, majiko sanifu na mkaa mbadala bidhaa ambazo zimetengenezwa na zinafundishwa kwenye kituo cha kutolea elimu ya mazingira Masasi. Picha na Godbless Lucius