Radio Fadhila

Sumu kuvu chanzo cha upungufu wa nguvu za kiume

1 June 2025, 4:54 PM

Mahindi yakiwa yameathiriwa na Sumu kuvu. Picha na Google

 “Tatizo watanzania wengi wanatumia mazoea kwenye shughuli za kilimo, hili tumekutana nalo kwenye maeneo mengi nchini, wanavuna mahindi wanatupa chini (ardhini) kama njia ya kukausha, hii inasababisha uzalishaji  fangasi wanaosababisha Sumukuvu”

Na  Neema Nandonde

Jamii wilayani Masasi mkoani Mtwara imeshauriwa  kuzingatia  kanuni bora  za kilimo na  namna nzuri ya  kuhifadhi  chakula ili kuepuka fangasi  zinazosababisha  sumu kuvu, ambayo ina athari kubwa kwa afya ya binaadam ikiwemo kwenye mfumo wa uzazi.

Hayo yameelezwa Mei 27, 2025 na Afisa Usalama  wa  Chakula  kutoka  Wizara  ya  Kilimo makao makuu Dodoma, Benny Rushunju alipokuwa akizungumza na redio Fadhila  baada  ya  kuhitimisha  mafunzo ya  siku 2, yaliyolenga kutoa elimu kuhusu Sumukuvu na uhifadhi wa chakula,  kwa mabalozi na viongozi wa kijamii takribani  600  kutoka wilayani Masasi yaliyofanyika katika ukumbi wa halmashauri ya wilaya ya Masasi.

Rushunju amesema  kuwa  miongoni mwa athari  za  Sumu kuvu ni pamoja kansa ya koo, udumavu, na  upungufu wa nguvu  za  kiume, huku akionya  kuhusu matumizi  ya  vyakula  vibichi vinavyochanganywa kwenye  mfuko mmoja ikiwemo karanga, korosho, mihogo na  nazi, mchanganyo unaojulikana  kwa jina maarufu Powerbank, kuwa vinaweza kusababisha  kuenea  kwa  Sumu kuvu kutoka  kwenye chakula kimoja kwenda  kwenye vyakula vingine.

Sauti ya Afisa Usalama  wa  Chakula  kutoka  Wizara  ya  Kilimo makao makuu Dodoma, Benny Rushunju

Kwa upande wake mgeni rasmi, ambaye pia ni mratibu wa mafunzo hayo kwa jimbo la Ndanda,  Mbunge  wa  jimbo hilo  Cecil Mwambe amewataka mabalozi waliopata  elimu  hiyo kwenda  kuisambaza kwa  wananchi, ili kuhakikisha  kuwa  wanafahamu  namna bora ya  kuhifadhi chakula na umuhimu wa kufuata kanuni bora za kilimo.

Sauti ya Mbunge wa jimbo la Ndanda Cecil Mwambe
Mbunge wa Jimbo la Ndanda Cecil Mwambe, akizungumza na mabalozi waliohudhuria mafunzo kuhusu Sumu kuvu. Picha na Edwin Mpokasye

Akizungumza kwa niaba ya mabalozi waliohudhuria mafunzo hayo, Diwani wa Kata  ya  Mwena  Nestory Chilumba amemshukuru Mbunge Mwambe kwa kuwezesha kupatikana kwa mafunzo hayo ambayo yatasaidia kulinda afya za wananchi wilayani Masasi.

Sumu kuvu ni kemikali sumu zinazozalishwa na fangasi wanaoingia  kwenye  mazao mbalimbali ikiwemo mahindi  na  karanga wakati yakiwa shambani au kwenye ghala.