Radio Fadhila

Heche: Kundi la G55 halitengui msimamo wa mkutano mkuu CHADEMA

11 April 2025, 2:06 PM

Makamu mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) John Heche akizungumza kwenye kipindi cha Asubuhi cha Morning Booster kinachorushwa na redio Fadhila. Picha na Godbless Lucius

Hata chama cha CHADEMA kikifanikiwa kushika dola, kisipotendenda haki kwa watanzania sisi kama wanachama  tutakemea na kuhitaji mabadiliko

Na Neema Nandonde

Makamu mwenyekiti  wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo  (CHADEMA) taifa  John Heche, amesema kuwa chama  hicho kinafuata misingi ya  katiba  hivyo kuundwa kwa kundi la  wanaojiita  G55 wao hawahusiki  nalo, na bado wataendelea kusisitiza msimamo uliotolewa na mkutano mkuu wa CHADEMA kuhusu  kampeni ya No Reforms No Election.

Ameyasema hayo April 8, 2025 alipokuwa akizungumza kwenye  kipindi cha asubuhi  cha Morning Booster  kinachorushwa  na  redio Fadhila, ambapo amesisitiza kuwa  msingi wa  kampeni ya  no reforms  no Election ni pamoja na  kudai mabadiliko ya  tume  huru ya taifa ya  uchaguzi (INEC), kwa kile alichokieleza kuwa mabadiliko hayo yatapelekea  uchaguzi  kuwa huru na wa haki.

Aidha amesema kuwa hata chama cha CHADEMA kikifanikiwa kushika dola, kisipotendenda haki kwa watanzania, wao kama wanachama  watakemea na kuhitaji mabadiliko.

Sambamba  na  hayo, Heche amewatoa wito kwa  wananchi kuhamasika kujaza fomu zinazolenga kupinga uchaguzi (petition form) endapo hakutakuwa na mabadiliko wanayoyahitaji, fomu ambazo zitapelekwa  kwa wananchi na zikisainiwa na wananchi million 15, zitapelekwa  serikalini na kwenye vyombo vingine husika  ndani na  nje ya nchi,  ili kuwasilisha maoni hayo ya  wananchi  juu  ya madai  ya  kutofanyika kwa uchaguzi mkuu kwakuwa  hakuna mabadiliko kwenye INEC.