Radio Fadhila

Hospitali ya Sokoine yakanusha kuukataa mwili

12 March 2025, 9:10 PM

Picha na Google

Kitendo kinachoelezwa kama ‘kukataliwa’ kimesababishwa na ndugu wa marehemu kupewa maelekezo ya kwanza yasiyo sahihi, kutoka kwa mhudumu aliyewataka  kwenda moja kwa moja kwenye geti dogo la kuingilia mochwari.

Na Neema Nandonde

Kufuatia mwanamke aliyejulikana kwa jina la Rukia Said, mkazi wa wilaya ya Kilwa mkoani Lindi, anayekadiriwa kuwa na umri wa  miaka 25-30,  kukutwa na  umauti ndani ya basi la abiria huku mashuhuda wakisema  kuwa mwili wake ulikataliwa kuingizwa Mochwari, Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Sokoine Dkt. Shadrack Msasi ametolea ufafanuzi suala  hilo.

Tukio hilo limetokea Machi 11, 2025 ambapo marehemu huyo amefariki akiwa  kwenye basi na  alikuwa akisafirishwa kutoka Kilwa  kuelekea Hospitali ya Rufaa mkoani Lindi – Sokoine kwa lengo la kupatiwa matibabu.

Kwa mujibu wa Mashuhuda, Mwili wa marehemu ulipofikishwa Hospitali, ulikataliwa kuingizwa ndani na kutelekezwa barabarani, huku ndugu wakiendelea kuomba msaada kutoka kwa wasamaria wema ili kurejea makwao kwa shughuli za mazishi.

Wameeleza kuwa sababu za kukataliwa kwa mwili huo, ni kukosekana kwa kitanda cha kubeba mwili na kuingizwa mochwari, jambo ambalo liliondosha matumaini ya kupatiwa huduma.

Akitolea  Ufafanuzi, Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa mkoani Lindi-Sokoine Dkt. Shadrack Msasi amekiri kutokea kwa sintofahamu hiyo, licha ya kukanusha kuwa, hospitalini hapo hawana utaratibu wa kakataa mwili kuingizwa ndani, bali kitendo kinachoelezwa kama ‘kukataliwa’ kimesababishwa na ndugu wa marehemu kupewa maelekezo ya kwanza yasiyo sahihi, kutoka kwa mhudumu aliyewataka  kwenda moja kwa moja kwenye geti dogo la kuingilia  Mochwari.

Baada ya  maelekezo  hayo, wakati basi hilo la abiria  limeshashusha mwili na  kuendelea na  safari yake, baadae  walipewa maelekezo ya kurejesha mwili huo geti kubwa, ili ufanyiwe vipimo kabla ya kupelekwa mochwari, jambo ambalo ndugu walikataa.

Amesema  licha  ya  kutumia muda  mrefu kuwashauri wapiti  geti kubwa kwaajili ya uchunguzi zaidi, ndugu wao waliendelea  kukataa na  hatimaye wakakodi gari dogo na kuuweka  mwili kwaajili ya kuusafirisha kuelekea  nyumbani kwao.

Aidha, amekana taarifa ya kukosekana kwa vitanda katika Hospitali hiyo kama taarifa zilizovyotolewa na kuongeza kuwa, vifaa vyote vinapatikana na huduma zote za msingi zinatolewa kwa uhakika.

Mpaka mwili wa marehemu unaondolewa eneo la tukio bila ya, wasamaria wema wakiongozwa na jopo la madereva wa bodaboda Manispaa ya Lindi, walikusanya kiasi cha shilingi 101,100/= zilizokabidhiwa kwa ndugu pamoja na jeneza, ili kuhifadhi mwili wakati na baada ya kurejea makwao.