Butiama FM Radio

RC Mara aagiza mikakati madhubuti kukabili Mvua za El Niño

12 September 2026, 7:00 am

Mkuu wa Mkoa wa Mara, Brigedia Jenerali Evans Alfred Mtambi, akizungumza na Kamati ya Maafa ya Mkoa pamoja na kamati za maafa katika ngazi mbalimbali kutekeleza mikakati ya kukabiliana na maafa katika maeneo yao kwa lengo la kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na mvua kubwa , kufuatia taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, (TMA) Picha na Amos Marwa

Tumepokea utabiri unaoonesha uwepo wa mvua za wastani hadi juu ya wastani katika Mkoa wa Mara. Hivyo, nawaagiza wajumbe wa Kamati ya Maafa ya Mkoa pamoja na kamati za maafa katika ngazi zote kuhakikisha wanachukua hatua za tahadhari mapema katika maeneo yao, kwa lengo la kulinda maisha ya wananchi, mali zao na mazingira. Aidha, Ofisi ya Afisa Madini Mkazi ihakikishe inafanya ukaguzi wa migodi yote na kubaini maeneo yenye viashiria vya hatari, ili hatua stahiki zichukuliwe kabla ya madhara kutokea.”Mkuu wa Mkoa wa Mara, Brigedia Jenerali Evans Alfred Mtambi

Na Amos Marwa

Mkuu wa Mkoa wa Mara, Brigedia Jenerali Evans Alfred Mtambi, ameiagiza Kamati ya Maafa ya Mkoa pamoja na kamati za maafa katika ngazi mbalimbali kutekeleza mikakati ya kukabiliana na maafa katika maeneo yao, kwa lengo la kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na mvua kubwa zinazotarajiwa kunyesha.

Akizungumza wakati wa kikao cha Kamati ya Maafa ya Mkoa wa Mara, Mtambi amesema utabiri unaonesha kuwa mvua hizo zinatarajiwa kuwa za kiwango cha wastani hadi juu ya wastani, hivyo kuwataka wananchi kuchukua tahadhari mapema kwa kulinda maisha yao, mali na mazingira yanayowazunguka.

 Kamati ya Maafa ya Mkoa pamoja na kamati za maafa katika ngazi mbalimbali kutekeleza kwaajili ya kikao hicho chakuweka mikakati ya pamoja ili kukabiliana na maafa yanayoweza kutokea kutokana na mvua hizo. Picha na Amos Marwa

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa ameiagiza Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mara kufanya ukaguzi katika migodi ya madini, ili kubaini maeneo yenye hatari kwa maisha na mali za wachimbaji, na kuchukua hatua stahiki za kuzuia madhara yanayoweza kujitokeza.

Kikao hicho ni sehemu ya maandalizi ya Mkoa wa Mara katika kukabiliana na athari za mvua hizo, kufuatia taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, TMA, inayoutaja Mkoa wa Mara miongoni mwa mikoa inayotarajiwa kuathirika zaidi na hali ya hewa ya El Niño inayotarajiwa kuanza mwishoni mwa Septemba 2026.

Sehemu ya Kamati ya Maafa ya Mkoa pamoja na kamati za maafa katika ngazi mbalimbali wakimsikiliza kwamakini Mkuu wa Mkoa wa Mara, Brigedia Jenerali Evans Alfred Mtambi kuhusu mikakati ya kukabiliana na maafa yanaweza kutokea kutokana na mvua hizo za el nino. Paicha na Amos Marwa