Butiama FM Radio
Butiama FM Radio
4 July 2026, 7:48 am

“Nawataka vijana na wananchi wote kulinda amani, umoja na utulivu wa nchi, kwa sababu mazingira ya amani ndiyo msingi wa maendeleo endelevu. Bila amani, hatuwezi kujenga uchumi imara wala kufanikisha maendeleo tunayoyahitaji kama taifa.”Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba
Na Amos Marwa
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, ameihakikishia jamii ya Wilaya ya Butiama mkoani Mara kuwa Serikali itachukua hatua za haraka kuboresha barabara za ndani ambazo zimekuwa hazipitiki, ili kurahisisha usafiri na usafirishaji wa bidhaa pamoja na huduma za kijamii.
Akizungumza leo katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Butiama, Dkt. Nchemba amesema Serikali imedhamiria kuhakikisha wananchi wanapata miundombinu bora inayochochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Aidha, amemuelekeza Meneja wa TARURA Wilaya ya Butiama kwa kushirikiana na Meneja wa TARURA Mkoa wa Mara kukamilisha usanifu wa barabara hizo ndani ya kipindi cha mwezi mmoja ili hatua za ujenzi na ukarabati zianze kwa wakati.

Waziri Mkuu pia amewataka wananchi wa Butiama kuendelea kulinda amani, umoja na utulivu wa nchi, akisisitiza kuwa mazingira ya amani ndiyo msingi wa maendeleo endelevu, Amesema ni wajibu wa kila mwananchi kulinda miundombinu ya umma na kujiepusha na vitendo vya uchochezi vinavyoweza kuhatarisha usalama na maendeleo ya taifa.
Ziara ya Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba mkoani Mara ni ya siku tano, ikiwa na lengo la kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo pamoja na kusikiliza na kutatua kero za wananchi.
