Butiama FM Radio
Butiama FM Radio
21 June 2026, 7:46 am

“Hakuna mfanyabiashara anayepaswa kupuuza kampeni hii ya usafi. Wale ambao hawakuhudhuria leo, majina yao yaandikwe kwa ajili ya kuchukuliwa hatua za kisheria,“ Mkuu wa Wilaya ya Butiama, Thecla Mkuchika.
Na Amos Marwa
Mkuu wa Wilaya ya Butiama, Thecla Mkuchika, amezindua rasmi kampeni ya usafi wa mazingira ya kila Jumamosi ijulikanayo kama “Ondoa Taka Butiama”, akisema hatua hiyo inalenga kujenga utamaduni endelevu wa usafi na kuhakikisha mazingira ya wilaya hiyo yanakuwa salama na yenye afya kwa wananchi.
Akizungumza wakati wa uzinduzi uliofanyika katika Kijiji cha Butiama, Mkuchika alielekeza viongozi wa halmashauri, kata na vijiji kusimamia kikamilifu utekelezaji wa sheria ndogo za usafi wa mazingira, huku akisisitiza kuchukuliwa hatua kwa watu wote watakaobainika kutupa taka hovyo katika maeneo ya umma.
Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Butiama, Albinus Sasita, aliwataka wananchi kudumisha usafi katika maeneo ya biashara na makazi yao ili kuepuka magonjwa ya mlipuko yanayoweza kutokea ikiwemo kipindupindu .

Wananchi wa Butiama wamepokea kampeni hiyo kwa matumaini makubwa, wakiahidi kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wake. Kampeni ya “Ondoa Taka Butiama” inatarajiwa kufanyika kila Jumamosi kwa ushirikiano wa wananchi, viongozi na wadau mbalimbali wa maendeleo kwa lengo la kuimarisha usafi wa mazingira na afya ya jamii.
