Butiama FM Radio

Wavamizi wachoma nyumba Muhunda

30 May 2026, 2:50 pm

Sehemu ya ukuta wa Nyumba ya Bwana David Wanzagi Nyerere iliyochomwa moto na watu wasiojulikana na kumjeruhi mlinzi na kupora sehemu ya mali zilizokuwemo ndani. picha na Oscar Mwakipesile

Tulikuwa na uzinduzi wa albamu ya muziki ambayo ilikuwa inafanyika katika sehemu yangu ya biasahara tulimaliza usiku na tulirejea saa tisa usiku tukiwa na mke wangu na kukuta nyumba imechomwa moto” David Wanzagi Nyerere

Na Amos Marwa

Watu wasiojulikana wamevamia nyumba ya Bw. David Wanzagi Nyerere, mkazi wa kitongoji cha Muhunda, Kata ya Butiama, Wilaya ya Butiama, na kusababisha uharibifu mkubwa kwa kuiba baadhi ya vitu vya thamani pamoja na kuchoma moto nyumba hiyo. Katika tukio hilo, mlinzi wa nyumba hiyo alijeruhiwa na watu hao kabla ya kutekeleza uhalifu wao.

Kwa mujibu wa Bw. Davidi Wanzagi Nyerere, yeye pamoja na mkewe hawakuwepo nyumbani wakati tukio hilo likitokea, kwani walikuwa katika shughuli zao za biashara. Alisema waliporejea nyumbani usiku walikuta nyumba ikiwa imeteketea kwa moto huku mali zote zilizokuwemo ndani zikiwa zimeteketea.

Sauti ya Bw. David Wanzagi Nyerere akielezea jinsi hali ilivyokuwa baada ya kukuta nyumba yake imechomwa moto na watu wasiojulikana

Akizungumzia tukio hilo, shahidi wa tukio James Wanzagi amewataka wananchi kujitafakari kuhusu sababu zinazosababisha matukio ya aina hiyo kujirudia mara kwa mara katika eneo hilo. Amesema kuna umuhimu wa jamii kushirikiana katika kudumisha amani na usalama ili kuzuia vitendo vya uhalifu.

Sauti ya James Wanzagi akielezea mfululizo wa matukio hayo katika mtaa huo na kuwataka wananchi wenzake kujitathimini juu ya matukio hayo

Naye Balozi wa mtaa huo, Yohana Magembe Joackimu, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuwataka wananchi kufuata sheria na taratibu pale wanapokuwa na malalamiko dhidi ya mtu yeyote. Amesisitiza kuwa kulipiza visasi kwa kuchoma mali za watu si suluhisho na kwamba wahusika wanapaswa kuchukuliwa hatua za kisheria.

Sauti ya mwenyekiti wa mtaa huo Yohana Magembe Joackimu akidhibitisha kutokea kwa tukio hilo

Wakati huo huo, Bw. Davidi amesema anatarajia kulifikisha suala hilo katika vyombo vya polisi kwa hatua zaidi za uchunguzi.

Sehemu ya dirisha la Nyumba ya Bwana David Wanzagi Nyerere iliyochomwa moto na watu wasiojulikana, kumjeruhi mlinzi na kupora sehemu ya mali zilizokuwemo ndani. picha na Oscar Mwakipesile