Butiama FM Radio

Dkt. Mahera asikiliza kero za wananchi Kukirango

17 July 2026, 10:25 am

Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles, akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Madaraka senta Kata Kukirango katika ziara ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo na kusikiliza kero za wananchi. picha na Mtandao

Nimepokea kero na maoni ya wananchi kuhusu huduma za maji, umeme, barabara na ujenzi wa soko la kisasa. Nitazifuatilia kwa karibu kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Butiama pamoja na wadau mbalimbali ili kuhakikisha changamoto hizo zinapatiwa ufumbuzi na wananchi wanaendelea kupata huduma bora.”Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles

Na Amos Marwa

Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles, ameendelea na ziara yake ya kikazi katika Kata ya Kukirango kwa kukagua miradi ya maendeleo, kusikiliza kero za wananchi na kuhamasisha utoaji wa huduma za kijamii. Ziara hiyo imeanza kwa kukabidhi vifaa maalum kwa wanafunzi wenye ualbino kupitia Idara ya Elimu ya Halmashauri ya Wilaya ya Butiama, kabla ya kufanya kikao na viongozi wa AMCOS kujadili maendeleo ya ushirika, kilimo na masoko ya mazao.

Katika ziara hiyo, Dkt. Mahera pia ametembelea nyumba ya kihistoria ya TANU iliyohusishwa na harakati za Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kuelekea Azimio la Arusha. Aidha, alikagua maendeleo ya ujenzi wa Kituo cha Afya Kiabakari pamoja na Ofisi ya CCM Tawi la Kiabakari.

Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles akikabidhi vifaa maalum kwa wanafunzi wenye ualbino kupitia Idara ya Elimu ya Halmashauri ya Wilaya ya Butiama. picha na Mtandao

Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika Madaraka senta ,Kijiji cha Kiabakari, Dkt. Mahera alisema amepokea kero na maoni ya wananchi kuhusu huduma za maji, umeme, barabara na ujenzi wa soko la kisasa, huku akiahidi kuzifuatilia kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Butiama pamoja na wadau mbalimbali.

Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles alivalia kofia nyeupe akiwa ameambatanana na maofisa wengine, akikagua maendeleo ya ujenzi wa Kituo cha Afya Kiabakari. picha na Mtandao

Dkt. Mahera amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuimarisha huduma za wananchi nchini. Vilevile, amewashukuru viongozi na wananchi wa Kata ya Kukirango kwa ushirikiano na mapokezi mazuri waliompatia wakati wa ziara hiyo.

Baadhi ya viongozi wa vyama vya ushirika (AMCOS) wakimsikiliza kwa makini Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles alipokutana na viongozi hao kujadili maendeleo ya ushirika, kilimo na masoko ya mazao. picha na Mtandao