Butiama FM Radio

Dkt. Mahera akagua miradi, asikiliza kero za wananchi Butiama

17 July 2026, 9:54 am

Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles akizungumza na wananchi wa Kyatungwe na Kiawazaru ambapo amepokea  kero, maoni na ushauri kuhusu huduma mbalimbali za  kijamii. Picha na Mtandao

“Nitashirikiana na Serikali pamoja na wananchi kuhakikisha miradi ya maendeleo inakamilika kwa wakati na kwa ubora unaohitajika, ili huduma muhimu ziendelee kuwafikia wananchi wa Jimbo la Butiama “Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles

Na Amos Marwa

Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles ameendelea na ziara yake ya kikazi kwa kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo na kusikiliza kero za wananchi katika Kata ya Kyatungwe.

Katika ziara hiyo  Dkt. Mahera amekagua barabara ya Sakya–Mayani (Kyatung we–Store), ujenzi wa Zahanati ya Nyamagana unaotekelezwa kwa nguvu za wananchi, Shule ya Sekondari Kyatungwe, kivuko cha Mubisaka pamoja na ujenzi wa matundu 12 ya vyoo katika Shule ya Msingi Kiawazaru.

Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles alievaa kofia nyeupe akiwa ameambatana na maofisa wengine akiwa ametembelea Shule ya Sekondari Kyatungwe . picha na Mtandao

Mbali na ukaguzi wa miradi hiyo, Mbunge huyo amekutana na wananchi wa Kyatungwe na Kiawazaru ambapo amepokea  kero, maoni na ushauri kuhusu huduma mbalimbali za  kijamii. Baadhi ya changamoto zilizokuwa ndani ya uwezo wa viongozi wa eneo hilo zimepatiwa  ufumbuzi papo hapo, huku nyingine zikichukuliwa kwa ajili ya kufuatiliwa na kutafutiwa suluhisho.

Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles alievalia shati jeupe na kofia nyeupe akikabidhi Mashine ya kunakili nyaraka (Mashine ya fotokopi) katika ziara yake iliyofanyika Kata ya Kyatungwe. picha na Mtandao.

Akizungumza katika ziara hiyo, Dkt. Mahera amesema ataendelea kushirikiana na Serikali pamoja na wananchi kuhakikisha miradi ya maendeleo inakamilika kwa wakati, kwa ubora unaohitajika na kwamba huduma muhimu zinaendelea kuwafikia wananchi wa Jimbo la Butiama.

Mbunge wa Jimbo la Butiama, Dkt. Wilson Mahera Charles akiwa ametembelea kivuko cha Mubisaka wakati wa ziara hiyo. picha na Mtandao