Radio Fadhila

NHC yapongezwa ujenzi wa kituo cha biashara Masasi

19 May 2025, 11:28 AM

Mradi wa ujenzi wa Kituo cha Biashara Masasi (Masasi Comercial Complex) kilichopo halmashauri ya mji Masasi. Picha na Godbless Lucius

Mradi wa Kituo cha Biashara Masasi (Masasi Comercial Complex) umelenga kuboresha huduma kwa jamii na wafanyabiashara ndani na nje ya wilaya ya Masasi

Na Neema Nandonde

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa kwa mwaka 2025, Ismail Ali Ussi, amelipongeza Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwa kujenga Kituo cha Biashara Masasi (Masasi Commercial Complex) katika halmashauri ya Mji wa Masasi mkoani Mtwara.

Ametoa pongezi hizo Mei 18, 2025 wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi katika ujenzi wa mradi wa huo, ambapo amesema kuwa kituo hicho kitarahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi sehemu moja, ikiwemo huduma za kifedha.

Sauti ya Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa kwa mwaka 2025 Ismail Ali Ussi

Kwa upande wake Meneja wa Mradi huo Godfrey Mkumbo, amesema jengo hilo la biashara linakadiriwa kugharimu jumla ya Shilingi 2,711,652,080.22 hadi kukamilika kwake, ambapo tayari kiasi cha Shilingi 1,450,718,159.94 kimeshatumika na unatarajiwa kukamilika  mwezi Septemba mwaka huu.

Sauti ya Meneja wa mradi wa ujenzi wa Kituo cha Biashara Masasi, Godfrey Mkumbo

Ukiwa katika Halmashauri ya Mji Masasi, Mwenge wa Uhuru umekagua miradi yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni tatu na kukimbizwa umbali wa km 78.0, ambapo umepitia miradi sita (Miradi miwili imezinduliwa, miradi miwili imewekewa mawe ya msingi na miradi miwili imekaguliwa).

Baadhi ya wanafunzi wakionesha na kuelezea ujumbe uliopo kwenye mabango yanayoelezea elimu inyaotolewa kwenye Kituo cha Elimu ya  Mazingira Masasi ambacho pia kimetembelewa na Mwenge wa Uhuru. Picha na Godbless Lucius
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Ismail Ali Ussi akiwa na Mkuu wa Wilaya ya Masasi Bi. Rachel Kassanda wakati wa uzinduzi wa nyumba za watumishi wa kituo cha afya Mtandi. Picha na Godbless Lucius

Mwenge wa Uhuru umehamasisha wananchi juu ya mapambano dhidi ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI, Malaria, Rushwa, Madawa ya kulevya na Lishe, ambapo kaulimbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2025 ni, “Jitokeze Kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 kwa Amani n a Utulivu ”.