Radio Fadhila

Watoto kutelekezwa kwa bibi sababu ongezeko la watoto mitaani

11 April 2025, 2:41 PM

Picha inayoaksi mtoto wa mitaani. Picha kwa hisani ya mtandao

Wazazi wengi huwapeleka watoto kwa ndugu akiwemo bibi au babu, pasi na kufuatilia maendeleo ya  watoto  hao au kuwapatia  mahitaji muhimu, jambo linalosababisha watoto kutoangaliwa ipasavyo na ndugu walioachiwa, na hatimaye kujikuta  wanajitafutia chakula, makazi na malazi mtaani.

Na Neema Nandonde

Imeelezwa  kuwa miongoni mwa sababu  zinazochangia ongezeko la  watoto wa mitaani wilayani Masasi mkoani Mtwara, ni baadhi ya  wazazi  kuwatelekeza watoto kwa bibi zao au kwa ndugu wengine, badala  ya  kuwalea wao wenyewe.

Hayo yameelezwa  na  Afisa Maendeleo  ya  Jamii Halmashauri ya Mji Masasi  Leila  Kasugulu alipokuwa akizungumza na Redio Fadhila kupitia kipindi cha Fadhila Mseto, April 11, 2025 kuhusu  maadhimisho  ya wiki ya mtoto wa mtaani.

Amesema wazazi wengi, huwapeleka watoto kwa ndugu akiwemo bibi au babu pasi na kufuatilia maendeleo ya  watoto  hao au kuwapatia  mahitaji muhimu, jambo linalosababisha watoto hao kutoangaliwa ipasavyo na ndugu walioachiwa na hatimaye kujikuta  wanajitafutia chakula, makazi na malazi mtaani.

Amesema  sababu nyingine ni ulevi uliopindukia wa wazazi au walezi, wazazi au walezi kufariki, wazazi kutengana  na kwa asilimia chache ni  tabia  ya utukutu wanayokuwa  nayo watoto wenyewe  hali inayosababisha watamani kuishi maisha huru mitaani.

Sauti ya Afisa maendeleo  ya  Jamii halmashauri ya mji Masasi  Leila  Kasugulu

Aidha ameeleza  kuwa halmashauri ya  mji  Masasi, inaendelea na jitihada za kuwaondoa watoto hao mitaani kwa kuwapeleka  kwa walezi wa kuaminika, wanaochaguliwa na idara ya ustawi wa jamii na  mashirika au taasisi nyingine binafsi zinazotetea haki za watoto, au kuwapeleka  kwenye vyuo vya ufundi ili waweze kujipatia ujuzi utakaowasaidia  kujipatia kipato halali.

Kilele cha  maadhimisho  hayo kitaifa, kitafanyika April 12, 2025 katika viwanja  vya  VETA mkoani Mtwara ambapo Waziri  wa  Maendeleo ya  Jamii, Jinsia, Wananawake  na  Makundi Maalum Dkt. Doroth Gwajima, anatarajiwa  kuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho hayo.